1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaRwanda

Mahakama Rwanda yaidhinisha marufuku ya mpinzani

20 Machi 2024

Mahakama ya Rwanda imetupilia mbali ombi la kurejesha haki ya kiraia ya kiongozi wa upinzani Victoire Ingabire.

https://p.dw.com/p/4dwjX
Rwanda Victoire Ingabire Kiongozi wa upinzani
Kiongozi wa upinzani Rwanda Victoire IngabirePicha: CYRIL NDEGEYA/AFP

Vile vile mahakama hiyo imetupilia mbali pia ombi la kumfutia hukumu zake za hapo awali alipokutwa na hatia ya ugaidi na kukana mauaji ya halaiki, na hivyo kumzuia kugombea katika uchaguzi wa urais wa Julai 15 mwaka huu.

Mkosoaji huyo mkubwa wa Rais wa Rwanda Paul Kagame, Ingabire alikaa gerezani kwa miaka minane kabla ya kupata msamaha wa rais mwaka 2018 uliofupisha kifungo chake cha miaka 15. Alikuwa ameomba Mahakama Kuu ya Kigali kufuta hukumu hizo na kumruhusu kugombea urais.

Kulingana na sheria za Rwanda, wagombea Urais hawapaswi kuwa waliwahi kuhukumiwa kifungo cha miezi sita au zaidi. Victoire Ingabire amesema hakubaliani na uamuzi huo huku akisema kuwa Mahakama si huru nchini Rwanda. Hata hivyo sheria inamruhusu tu kukata rufaa baada ya miaka miwili.