1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Israel yaanza kuvunja majengo ya UNRWA Jerusalem Mashariki

20 Januari 2026

Polisi nchini Israel imevamia makao makuu ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuwahudumia Wakimbizi wa Kipalestina, UNRWA na kuanza kubomoa majengo. Haya yameripotiwa leo na Umoja wa Mataifa pamoja na vyombo vya habari.

https://p.dw.com/p/578JZ
Mkutano na waandishi wa habari  - UNRWA - Philippe Lazzarini | UNRWA-
Mkuu wa shirika la UNRWA, Philippe Lazzarini Picha: Chris Emil Janssen/picture alliance

Vyombo hivyo vya habari vya Israel na Palestina vimethibitisha kuanza kwa ubomoaji wa majengo hayo.

Shirika la UNRWA katika ukanda wa Mashariki ya Kati pia limethibitisha kuwa maafisa wa Mamlaka ya Ardhi ya Israel walihusika kwenye operesheni hiyo.

Katika chapisho kwenye mtandao wa kijamii wa X, mkuu wa UNRWA  Philippe Lazzarini amelaani hatua hiyo na kuitaja kuwa "kiwango kipya cha ukiukaji wa wazi na wa makusudi wa sheria za kimataifa, ikiwa ni pamoja na haki na kinga za Umoja wa Mataifa, uliofanywa na taifa la Israeli."

Lazzarini amelitaja tukio hilo kama "shambulio ambalo halijawahi kutokea" dhidi ya Umoja wa Mataifa na kuonya kwamba linaweza kutokea kwa shirika lingine lolote.

Ameongeza kuwa hatua hiyo inapaswa kuchukuliwa kama tahadhari.