1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Inspekta wa polisi awauwa watu watano mjini Enugu

Amina Mjahid
21 Juni 2021

Polisi nchini Nigeria imesema inspekta mmoja wa jeshi la polisi ameuwa raia watano na kuwajeruhi wengine wanne katika tukio la ushambuliaji risasi katika tukio la hivi karibuni la vurugu kusini mashariki mwa nchi hiyo. 

https://p.dw.com/p/3vHpQ
Symbolbild | Nigeria | SWAT
Picha: AFP/Y. Chiba

Katika taarifa yake msemaji wa polisi Daniel Ndukwe amesema tukio hilo lilitokea siku ya Jumapili wakati inspekta huyo alipovamilia eneo la makaazi ya watu katika jimbo la Enugu, na kuanza kuwamiminia risasi wakaazi waliokuwepo.

Wale waliojeruhiwa wamepelekwa hospitalini kwa matibabu. Ndukwe amesema watu watano waliojeruhiwa vibaya, walithibitishwa kufariki na daktari waliokuwa kazini walipolekwa hospitalini na kwa sasa wamepelekwa katika vyumba vya kuhifadhia maiti wakisubiri kufanyiwa uchunguzi.

soma zaidi: Jeshi la Nigeria lakataa kutwaa madaraka

Msemaji huyo wa polisi, Daniel Ndukwe amesema afisa aliyetekeleza kisa hicho amekamatwa na tayari uchunguzi umeanzishwa wa kubaini sababu hasa ya kutekeleza mauaji hayo.

Eneo la kusini mashariki mwa Nigeria limeshuhudia ongezeko la mashambulizi dhidi ya maafisa wa polisi katika siku za hivi karibuni yaliyosababisha mauaji ya watu wengi wakiwemo maafisa wa polisi.

Kundi lililopigwa marufuku la waasi wanaopigania kujitenga kwa Biafra linalojiita wakaazi asili wa Biafra (IPOB) limekanusha mara moja kuhusika na shambulizi la Jumatatu.

Tamko la upande mmoja la kutangazwa kwa uhuru wa Jamhuri ya Biafra mwaka 1967 ulisababisha mapigano ya wenyewe kwa wenyewe yaliyodumu kwa miezi 30 yaliyosababisha mauaji ya zaidi ya watu milioni moja kutoka jamii ya Igbo, kabla vikosi vya serikali ya shirikisho kuusambaratisha uasi uliokuwepo.

Chanzo: reuters