1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

G7 wataka ukandamizaji ukome Myanmar

Mohammed Khelef
23 Februari 2021

Kundi la mataifa saba yenye nguvu za kiuchumi duniani, G7, limetaka kukomeshwa mara moja ukandamizaji na vitisho dhidi ya wapinzani wa mapinduzi ya kijeshi nchini Myanmar.

https://p.dw.com/p/3pkwi
Myanmar | Demonstration gegen Militärputsch
Picha: AP/picture alliance

Katika tamko lao la siku ya Jumanne (Februari 23), wanachama cha G7 walisema wanalaani vikali hatua ya jeshi kuwashambulia waandamanaji wanaopinga mapinduzi ya kijeshi ya tarehe 1 Februari. 

"Matumizi ya risasi za moto dhidi ya watu wasiokuwa na silaha hayakubaliki. Yeyote anayejibu maandamano ya amani kwa ghasia lazima awajibishwe," ilisema taarifa ya mawaziri wa mambo ya kigeni wa G7.

Kwenye tamko lao, walilitaka jeshi "kujiepusha na matumizi ya nguvu na kuheshimu haki za binaadamu na sheria za kimataifa."

Maandamano yageuka mauaji

Myanmar | Proteste nach Militärputsch
Maandamano dhidi ya jeshi yaendelea.Picha: AP Photo/picture alliance

Waandamanaji wanaopigania demokrasia wamekuwa wakiingia mitaani kwenye miji kadhaa ya Myanmar kwa wiki kadhaa sasa tangu jeshi lilipochukuwa madaraka tarehe 1 Februari, wakitaka kuachiliwa mara moja kwa kiongozi aliyepinduliwa Aung San Suu Kyi na Rais Win Myint.

Jeshi, ambalo limetangaza hali ya hatari na kuahidi kufanya uchaguzi ndani ya mwaka mmoja, limekuwa likitumia nguvu kuwakabili waandamanaji, ambapo hadi sasa waandamanaji watatu wameshauawa.

Waandamanaji waliingia tena mitaani siku ya Jumanne, ingawa kwa idadi ndogo kuliko ilivyoshuhudiwa siku ya Jumatatu ambapo kulikuwa na mgomo mkubwa wa kitaifa.

Jeshi linasema limechukuwa madaraka kwa sababu uchaguzi wa mwezi Novemba uliibiwa na kukiwezesha chama cha Aung San Suu Kyi, NLD, kilipata ushindi mkubwa, madai yanayokanushwa na tume ya uchaguzi.