1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

FC Cologne yafufua matumaini kubakia Bundesliga

Sekione Kitojo
22 Januari 2018

FC Cologne yajitutumua na kufufua matumaini kujinasua kushuka  daraja. Sakata  kuhusu Pierre-Emerick  Aubameyang linaendelea, kikao cha siri kinaendelea mjini Borussia Dortmund pamoja na viongozi wa  Arsenal.

https://p.dw.com/p/2rJW1
Fußball Bundesliga Hamburger SV - FC Köln Simon Terodde
Picha: Imago/DeFodi/R. Treese

Mchezo  wa  19  wa  Bundesliga umeleta  zaidi  mvuto katika  eneo  la  mkiani  mwa  msimamo  wa  ligi, ambapo Hamburg SV  ambayo  iko  katika  nafasi  ya  17 ikiwa nyumbani  iliikaribisha  FC Cologne  ambayo  wengi wanaitabiria  kuwa  imo  njiani  kuelekea  katika  daraja  la pili  baada  ya  kuwa  na  pointi 9  tu  kabla  ya  mchezo  wa jioni  ya  Jumamosi. FC Cologne ilihitaji  ushindi  kwa kila  hali ili  kujiweka  katika  nafasi  nzuri  ya  kupambana  kujitoa kutoka  katika  hatari  ya  kushuka  daraja. Na  ndivyo walivyofanya  dhidi  ya  Hamburg SV , kwa  ushindi  wa mabao 2-0.

1. Bundesliga - Hamburger SV vs FC Köln
Wachezaji wa akiba na viongozi wa FC Kolon wakishangiria ushindi mnono dhidi ya Hamburg SVPicha: Reuters/F. Bimmer

Baada  ya  ushindi  huo nahodha wa  FC Cologne Matthias Lehmann alisema.

„Tumeshinda hadi sasa michezo  mitatu  mfululizo. Hakuna aliyeweza kuamini. Ukishindwa  dhidi  ya  timu  ya  mwisho, kama  ilivyo  kwa  Hamburg leo, morali inashuka. Kwetu sisi morali iko juu. Ndio sababu  tunataka kuibeba  hali  hiyo katika mchezo  wa wiki  ijayo."

Hamburg imetengana na kocha  wake Markus Gisdol  na  tayari wamemteua  mchezaji  wao  wa  zamani Bernd Hollerbach kuwa kocha  wa  timu  hiyo.

HSV-Trainer Markus Gisdol
Kocha wa zamani wa hamburg Markus GisdolPicha: picture-alliance/dpa/A. Heimken

Werder Bremen  ambayo  nayo  imo katika  eneo  la  hatari  ya kushuka  daraja , ikiwa  nafasi  moja  tu  juu  ya  Hamburg SV katika  nafasi  ya  16  na  ikiwa  na  pointi 16 , moja  tu  zaidi  ya Hamburg , ilipigana  kiume  dhidi  ya  mabingwa  watetezi  na mabingwa  watarajiwa  Bayern  Munich  na  kukubali  kipigo  cha mabao 4-2 hali  ambayo haitoi  matumaini  makubwa  kwa Bremen  kubakia  pia  katika  daraja  la  kwanza. Hata  hivyo mshambuliaji  wa  Bayern Thomas Mueller  alikiri  kwamba mchezo  huo haukuwa  rahisi  kwa mabingwa  hao.

„Leo haikuwa  siku   yetu nzuri, ambapo mambo  yalikuwa yanakwenda tu. Mwanzoni  tulikuwa kidogo wavivu. Bremen walifanya  vizuri sana, katikati walifunga njia zote. Tuliwaruhusu Bremen kutumia  mbinu  zao na  kutushambulia kwa  urahisi kabisa. Lakini  mwishoni  tuliweza  baadae  kuchukua  hatamu za mchezo huo."

Deutschland Bayern München gegen Werder Bremen | Thomas Müller
Mshambuliaji wa Bayern Munich Thomas Mueller Picha: Reuters/M. Rehle

Bayer yachupa

Bayer Leverkusen baada  ya  kipigo  cha mabao 3-1  dhidi  ya mabingwa  Bayern Munich  katika  mchezo  wa  18  wa Bundesliga, ilizinduka  mara  hii  katika  mchezo  wa  19  na kuivuruga  Hoffenheim  siku  ya  Jumamosi  kwa  kuishindilia mabao 4-1 nyumbani. Bayer Leverkusen  imechupa  toka  nafasi ya  tano wiki  iliyopita  hadi  nafasi  ya  pili  ya  msimamo  wa  ligi kwa  kuwa  na  pointi 31, ikiwa  ni  pointi 16 nyuma  ya  viongozi wa  ligi  hiyo  Bayern Munich. Kocha  wa  Leverkusen Heiko Herrlich  hata  hivyo  alisema  mchezo  huo  haukuwa  rahisi kama  matokeo  yanavyoonesha.

„Iwapo  kabla  ya  mchezo mtu angesema tungetoka  na  pointi moja, ningekubali  haraka sana. Hoffenheim ni  timu  ngumu sana. Nafikiri  leo tumecheza  vizuri  sana . Nimefurahi  sana kupata  pointi tatu."

FC Schalke 04 imefanikiwa  kutoka  suluhu  jana  Jumapili  dhidi ya  Hannover 96  kwa  kufungana  bao 1-1, lakini mchezo  huo uligubikwa  na  hali  ya  mashabiki  wa  Schalke kupiga  miluzi uwanjani  wakimshutumu  mchezaji  wao  wa  kati Leon Goretzka kutangaza  kwamba  anahamia  katika  klabu  ya  Bayern  Munich msimu  ujao.

Fußball FC Schalke 04 v 1. FSV Mainz 05 - 1. Bundesliga Torjubel 1:0
Leon Goretzka mchezaji anayehamia Bayern Munich msimu ujaoPicha: Imago/Team 2

Hasira  za  mashabiki  wa  Schalke ni  pamoja  na kujivuta kwa  Leon Goretzka  kutangaza  na  mapema  nia  yake hiyo na  hatimaye  kuinyima  mapato klabu  ya  Schalke , baada ya  kutangaza  nia  hiyo  akiwa  mkataba  wake  unafikia  mwisho na  kuwa  mchezaji  huru  na  kwa  hiyo  kuondoka  bila Bayern kulipa chochote  kwa  Schalke. Hata  hivyo Goretzka amesema anatambua hisia za  mashabiki  wa Schalke.

„Sihitaji kumdanganya mtu  na  hata kujidanganya mimi  binafsi. Ilikuwa  ni  hali  tofauti  kabisa, bila  shaka. Kwamba  timu haikuvurugika, na  nimefurahi sana. Kwamba  mashabiki  wengi wameonesha kutoridhishwa kwa kupiga  miluzi ni  kitu kinachoeleweka  na  kwa  kuwa  kila kitu kilikuwa ndani  ya mipaka yake, na  ndivyo  ilivyokuwa, kwa  hiyo  kila kitu kilikuwa sawa."

Dortmund yaporomoka

Borussia  Dortmund imeporomoka  hadi  nafasi  ya 6 kutoka nafasi  ya  tatu baada  ya  kutoka  sare ya  pili  mfululizo  siku  ya Ijumaa   dhidi  ya  Hertha Berlin. RB Leipzig ilipokea  kipigo  cha mabao 2-1  dhidi  ya  Freiburg  na  kuporomoka  hadi  nafasi  ya 4.

Sakata  la  mvutano  uliojitokeza  kati  ya  Borussia  Dortmund  na mshambuliaji  wake  nyota  Pierre-Emerick Aubameyang  kutaka kuhamia  klabu  nyingine linaendelea. Mara  hii  lakini  wahusika kutoka  klabu  ya  Arsenal  wamewasili  mjini  Dortmund  kufanya mazungumzo  ya  siri  na  viongozi  wa  klabu  hiyo  ili kukamilisha  uhamisho  wa  mchezaji  huyo  ambaye anaonekana  hana  hamu tena kucheza  katika  kikosi  hicho cha BVB.

Fussball Pierre-Emerick Aubameyang und Arsenal
Pierre-Emerick Aubameyang anayetaka kwa kila hali kuihama BVBPicha: picture alliance/SvenSimon/E. Kremser

Kwa upande mwingine  Alexis Sanchez  wa  Arsenal anaripotiwa  kuwa atakuwa mchezaji  wa  Manchester United kuanzia  leo  baada  ya  kutolewa  picha  inayomuonesha mchezaji  huyo  kutoka  Chile  akiwa  katika  uwanja  wa  Old Trafford akivalia  jezi  ya  klabu  hiyo.

Sanchez , mwenye umri  wa  miaka  29 , anatarajiwa  kuwa mchezaji  wa  Man United  ambaye  analipwa  mshahara mkubwa  zaidi kuliko  wote , ambapo  mshahara  wake unakadiriwa  kufikia  zaidi  ya  pauni za  Uingereza  500,000 kwa wiki.

Kocha  wa  Arsenal Arsene Wenger  na  Jose Mourinho wa Manchester United wamesema  wanatarajia  makubaliano  ya pande  mbili baina  ya  vilabu  hivyo  vya  Premier League yatafanikiwa.

Fußball UEFA Europa League Arsenal - 1. FC Köln
Mchezaji anayetarajiwa kujiunga na Manchester United kutoka Arsenal Alexis SanchezPicha: Reuters/Action Images/J. Sibley

Wakati  huo  huo  Henrick Mikhtariyan amekamilisha  uhamisho wake  kutoka  Manchester United  kwenda  Arsenal. Mikhitariyan anaondoka  Manchester United  baada  ya  kushindwa  kupata namba  ya  kudumu  katika  kikosi  cha  Jose Mourinho.

 

Mwandishi :  Sekione  Kitojo / ape / rtre / dpae

Mhariri: Iddi Ssessanga