1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bunge la lapinga kujumuishwa makundi ya wenye silaha jeshini

Sudi Mnette
9 Novemba 2022

Bunge la taifa la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, limepiga marufuku ujumuishaji wa makundi yenye kumiliki silaha katika jeshi, polisi au idara nyingine yoyote ya usalama.

https://p.dw.com/p/4JHJo
Demokratische Republik Kongo | Unruhen in Beni
Picha: Alexis Huguet/AFP/Getty Images

Hayo yamejiri baada ya Rais Felix Tshisekedi kutoa wito wa kuhamasishwa dhidi ya uvamizi wa Rwanda, akisisitiza vijana kujiunga na jeshi la taifa ili kushinda vita. Na hivyo bunge limechukuwa hatua hiyo kama tahadhari, ili kuepusha kujipenyeza pamoja na madhara mengine yanayotokana na kuchanganyika ndani ya jeshi makundi yenye kumiliki silaha. Kwa maelezo kamili.

Katika pendekezo lake kuhusu kuibuka makundi yenye kumiliki silaha mashariki mwa nchi hii, bunge limesisitiza kuwa uvamizi unaoendeshwa na jeshi la Rwanda kupitia kundi la waasi la M23, umesababisha hasara nyingi za maisha ya binadamu pamoja na uporaji wa rasilimali, pia kuhamishwa maelfu ya Wakongomani na hivyo kuzorotesha zaidi hali ya kibinadamu ambayo tayari inatia wasiwasi.

Marufuku kali ya bunge la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo

Felix Tshisekedi | Präsident Demokratische Republik Konogo
Rais Felix Tshisekedi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya CongoPicha: Arsene Mpiana/AFP/Getty Images

Kwa kulinda jeshi na polisi wa kitaifa pamoja na vyombo vingine vya usalama dhidi ya kupenyeza kwa matokeo mengine mabaya yatokanayo na michakato ya mara kwa mara ya kuchanganyika jeshi na makundi yenye kumiliki silaha, bunge limepiga marufuku serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo kushirikiana, kutangamana au kufanya mazungumzo yoyote yanayolenga kujumuisha ndani ya idara hizo, watu kutoka makundi yenye kumiliki silaha.

Christophe Mboso ambae ni Spika wa Bunge la taifa anasema, "Kutokana na matokeo ya kura, pendekezo la kupiga marufuku kuchanganyika makundi ya magaidi na makundi mengine yenye kumiliki silaha ndani ya jeshi, polisi na idara za usalama za Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo limepitishwa".

Ngome ya waasi ya M23 yashambuliwa kutoka angani

Wakati hayo yakijiri, jeshi la Kongo limeendelea leo Jumatano na mashambulizi ya anga ambayo yalianza jana Jumanne dhidi ya ngome za waasi wa M23 katika baadhi ya maeneo za Rutshuru mkoani Kivu Kaskazini.

Miongoni mwa maeneo yaliyoshambuliwa na ndege hizo mbili za kivita za Sukhoi-25 ni Tshanzu na Runyonyi, wakati huko Bunagana, mji mhimu ulio mpakani na Uganda ambao unadhibitiwa na M23 kwa zaidi ya miezi minne, wakaazi wanavuka mpaka na kuingia Uganda.

Soma zaidi:DRC, Rwanda zakubaliana kusaka suluhisho

Upande mwengine, maelfu ya vijana kutoka Kivu Kaskazini na Ituri wameanza kujiunga na jeshi la taifa ili kuitikia wito uliotolewa na na Rais Félix Tshisekedi.

DW,  Kinshasa