1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Serikali ya Uingereza yachapisha athari za kukosa mkataba

Tatu Karema
12 Septemba 2019

Serikali ya Uingereza imechapisha waraka kuhusu matayarisho ya kukabiliana na hali inayoweza kujitokeza, ikiwa nchi hiyo itaondoka katika Umoja wa Ulaya bila makubaliano.

https://p.dw.com/p/3PRzw
UK Brexit | Parlament
Picha: AFP/HO

Katika waraka huo wa kurasa sita ambao ulitolewa tarehe 2 Agosti, serikali ya Uingereza inaonyesha maandalizi ya nchi hiyo kujiondoa katika Umoja wa Ulaya almaarufu Brexit bila ya makubaliano ifikapo tarehe 31 mwezi Oktoba ambapo inaonya kuweko kwa hali ya kucheleweshwa katika njia za vivukio, gharama ya juu ya umeme na athari katika usambazaji wa dawa na chakula.

Ripoti hiyo imesema kuwa hatua hiyo ya Brexit pia inatarajiwa kuibua machafuko ya kijamii kwa kuwa maandamano yatafanyika kote nchini humo na huenda yakatumia raslimali nyingi za idara ya polisi. Waraka huo unatoka katika mpango wa serikali wa Brexit bila ya mkataba iliyobandikwa jina, '' Operesheni nyundo ya njano'' na ilichapishwa jana baada ya wabunge kupiga kura ya kutaka itolewe hadharani.

Awali akijibu swali kutoka kwa mwanahabari kuhusu kura ya maamuzi iwapo chama chake cha Labour kitafanyia kampeini makubaliano ya kujiondoa katika Umoja wa Ulaya ama kusalia katika Umoja huo, kiongozi wa chama hicho Jeremy Corbyn alijibu, ''Tutajadiliana kuhusu mkataba mwafaka wa Brexit halafu kufanya maamuzi wakati huo. Jambo la msingi Zaidi ni kwamba raia wenyewe wataweza kufanya maamuzi hayo lakini hakutakuwa na Brexit bila mkataba na Umoja wa Ulaya na shida zote ambazo zinaweza kutatiza sekta ya utengenezaji bidhaa, usambazaji wa bidhaa za huduma za afya na uhuru wa watu kuendelea na shughuli zao za kawaida."

Katika ujumbe kupitiaukurasa wa Twitter, waziri kivuli anayehusika na masuala ya Brexit wa chama cha Labour Keir Starmer amesema kuwa waraka huo umethibitisha athari kubwa za mchakato wa Brexit bila kuwepo kwa mkataba  ambapo chama hicho kimeupinga. Starmer ameongeza kusema kuwa serikali imeonyesha hali ya kutojali kwa kujaribu kupuuza tahadhari hizi na kuzuia umma kuona ushahidi huo.

Ameendelea kusema kwamba Waziri Mkuu Boris Johnson sasa anapaswa kukiri kwamba hajakuwa na uwazi kwa raia wa Uingereza kuhusu athari za Brexit bila ya kuweko kwa makubaliano na kwamba sasa ndio wakati mwafaka kwa bunge kurejelea vikao vyake kuchunguza waraka huo na kuchukuwa hatua zinazohitajika kuzuia Brexit ya kiholela.

Serikali mjini London imesisitiza kuwa inarekebisha mtazamo katika waraka huo na kwamba haimaanishi ni ukadiriaji wa athari ama utabiri wa kile kinachotarajiwa kutokea: Wiki iliyopita, wabunge walipiga kura kuilazimisha serikali kutoa ripoti hiyo baada ya toleo lake kuonekana kimakosa