1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Brazil yakataa msaada wa G7 kuzima moto wa Amazon

Yusra Buwayhid
27 Agosti 2019

Brazil Jumatatu imekataa msaada wa kifedha wa dola milioni 20 wa kusaidia kuzima moto katika msitu wa Amazon kutoka kundi la (G7).

https://p.dw.com/p/3OXfX
Brasilien Waldbrände
Picha: picture-alliance/AP/E. Peres

Nchi za kundi la mataifa saba yenye uchumi mkubwa wa viwanda G7 zimeahidi msaada wa dola milioni 20 kupambana na moto huo wakati wakiwa katika mkutano wa kilele mjini Biarritz, Ufaransa. Lakini  Rais wa Brazil Jair Bolsonaro amemuambia Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron ashughulikie nchi yake na makoloni yake.

Macron ambaye alikuwa mwenyeji wa mkutano huo, aliwasisitizia wenzake kuwa wanapaswa kuupa kipaumbele moto unaowaka katika msitu wa Amazon. Mbali na fedha hizo, Uingereza kwa upande wake imeahidi kutoa dola milioni 12, na Canada itatoa dola milioni 11 pamoja na ndege za kuzima moto.

Onyx Lorenzoni, mkuu wa shughuli za ofisi ya rais wa Brazil ameiambia tovuti ya habari ya G1 kwamba wanashukuru lakini labda fedha hizo zitafaa zaidi kupanda miti na kuimarisha misitu barani Ulaya, huku rais Bolsonaro akisema hamna msaada unaotolewa bure.

"Macron ameahidi msaada kutoka nchi za kitajiri utumike Amazon. Kwa nini macho yao yote wameyaelekeza Amazon? Wanataka nini huko kwa muda mrefu?," amesema Bolsonaro.

Soma zaidi:G7 yaingilia kati moto wa Amazon 

Brasilien Präsident Jair Bolsonaro
Rais wa Brazil, Jair BolsonaroPicha: picture-alliance/dpa/E. Peres

Tatizo la ulimwengu

Macron alimjibu Bolsonaro kwa kusema kwamba japo kuwa sehemu kubwa ya Amazon imo ndani ya Brazil, lakini hili ni suala la ulimwengu na ujumbe wake kwa kiongozi huyo ni kwamba ulimwengu hautomruhusu kuangamiza kila kitu.

Waziri wa Mazingira wa Brazil Ricardo Salles awali aliwaambia waandishi habari kwamba wanaukaribisha msaada wa nchi za G7 ili kuukabili moto huo unaoteketeza ekari milioni 2.3 katika msitu wa Amazon. Lakini baada ya mkutano na Bolsonaro pamoja na mawaziri wake, serikali ya Brazil ilibadilisha msimamo wake.

Ingawa asilimia 60 ya msitu wa Amazon imo ndani ya Brazil, msitu huo mkubwa unasambaa pia katika nchi nyingine nane ikiwa ni pamoja na Guiana iliyowahi kuwa koloni la Ufaransa na sasa ni sehemu ya Ufaransa kisiasa na kisheria.

Bolsonaro ambaye ni mkosoaji mkubwa wa suala la mabadiliko ya tabianchi amekabiliwa na ukosoaji mkubwa kutoka nje na ndani ya nchi yake, kwa kuchelewa kwake kupambana na moto huo wa Amazon. Wengi hawakufurahishwa na uongozi wake katika suala hilo. Nchini mwake hivi karibuni, maelfu ya watu walimiminika barabarani kukemea uharibifu huo unaendelea katika msitu wa Amazon.

Soma zaidi: Brazil: Bolsonaro kupeleka jeshi kuzima moto Amazon

Chanzo: (afp,ap)