Algeria yafuzu, Sudan na Msumbiji watamba
29 Desemba 2025
Algeria imekuwa taifa la tatu kufuzu hatua ya mtoano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) baada ya kuibuka na ushindi wa 1-0 dhidi ya Burkina Faso mjini Rabat. Bao pekee la mchezo lilifungwa na nahodha Riyad Mahrez kupitia mkwaju wa penalti dakika ya 23, baada ya Rayan Aït‑Nouri kuangushwa ndani ya eneo la hatari.
Ushindi huo unaifanya Algeria kufikisha pointi sita baada ya mechi mbili za Kundi E, bila kuruhusu bao, na kuendeleza hadhi yao kama miongoni mwa wagombea wakuu wa taji. Mahrez sasa ana mabao matatu katika mashindano haya na jumla ya mabao tisa katika historia ya AFCON, rekodi ya taifa hilo.
Miongoni mwa mashabiki 18,522 waliokuwepo uwanjani alikuwapo gwiji wa Ufaransa Zinedine Zidane, aliyekuja kumtazama mwanawe, Luca Zidane, anayekipiga kama kipa wa Algeria.
Mchezaji bora wa mechi hiyo, Ibrahim Maza, alisema baada ya mechi, "Tulijua itakuwa ngumu, lakini tulipambana. Lengo letu lilikuwa kufuzu, na tumefanikisha.”
Sudan yaongeza matumaini ya kusonga mbele
Katika mchezo mwingine wa Kundi E, Sudan ilipata ushindi muhimu wa 1-0 dhidi ya Guinea ya Ikweta, bao likitokana na kujifunga kwa beki Saul Coco dakika ya 74. Jaribio la Luis Asue kuondoa mpira wa adhabu ulimgonga Coco na kujaa wavuni.
Ushindi huu ni wa pili kwa Sudan katika mechi 18 za AFCON tangu walipotwaa taji mwaka 1970. Timu hiyo inashiriki michuano hii licha ya nchi kukumbwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe tangu Aprili 2023.
Ivory Coast na Cameroon sambamba
Katika Kundi F, mabingwa watetezi Ivory Coast walilazimishwa sare ya 1-1 na Cameroon katika mchezo mkali uliochezwa Marrakesh.
Amad Diallo aliwapa Tembo uongozi dakika ya 51, akifunga bao lake la pili katika mashindano haya. Hata hivyo, Cameroon walisawazisha ndani ya dakika tano kupitia shuti la Junior Tchamadeu lililomgonga Ghislain Konan na kutikisa wavu.
Ivory Coast na Cameroon sasa zinaongoza kundi kwa pointi nne kila moja, zikifuatiwa kwa karibu na Msumbiji.
Msumbiji yaandika historia baada ya miaka 39
Msumbiji ilipata ushindi wake wa kwanza katika historia ya AFCON baada ya kuichapa Gabon 3-2 katika mchezo wa kusisimua mjini Agadir. Kabla ya ushindi huu, Mambas walikuwa wamecheza mechi 16 bila kushinda tangu walipoanza kushiriki mwaka 1986.
Kocha Chiquinho Conde alieleza hisia zake kwa fahari, "Huu ni ushindi wa kihistoria. Tulipitia changamoto nyingi, lakini leo tumethibitisha kuwa inawezekana.”
Mabao ya Msumbiji yalifungwa na Faisal Bangal, Geny Catamo, na Diogo Calila, huku Gabon wakipata mabao kupitia Pierre‑Emerick Aubameyang na Alex Moucketou‑Moussounda.