1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaVatican

Vatican yaendelea kupinga kubadilisha jinsia

Lilian Mtono
8 Aprili 2024

Vatican imetangaza hii leo kwamba upasuaji wa kubadilisha jinsia na watu kubeba mimba kwa ajili ya wengine kuwa ni ukiukwaji mkubwa wa utu wa binaadamu.

https://p.dw.com/p/4eYPZ
Vatikan Papst Franzikus Ostern
Picha: Andrew Medichini/AP Photo/picture allliance

Vatican imeongeza kuwa vitendo hivyo ni sawasawa na vitendo vya utoaji mimba na kumsaidia mgonjwa kufa, masuala yanayopingana na mpango wa Mungu kwa maisha ya binaadamu.

Ofisi inayohusiana na mafundisho ya Kanisa Katoliki imesema hayo katika azimio linalohusu kitisho dhidi ya ubinadamu, lililoandaliwa kwa miaka mitano, ambalo baada ya kupitiwa upya miezi ya hivi karibuni, Kiongozi wa Kanisa, Papa Francis aliagiza kuchapishwa.

Kwenye azimio hilo, Vatican kwa mara nyingine imepinga nadharia ya jinsia ama wazo la kubadilisha jinsia ya mtu, kwa kusema Mungu amemuumba mwanaume ama mwanamke wakiwa tofauti kibaiolojia na viumbe tofauti na kuonya watu kutojifanya Mungu kwa kuamua vinginevyo.   

Wanaharakati wa wanaojihusisha na mapenzi ya jinsia moja kwenye kanisa hilo mara moja waliuokosoa waraka huo kama uliopitwa na wakati, wenye madhara na unaopingana na lengo la awali la kuitambua hadi isiyokoma kwa watoto wote wa Mungu.