Utambue muungano wa CORD
27 Februari 2013Muungano wa CORD unaoongozwa na Waziri Mkuu Raila Odinga na mgombea mwenza Makamu wa Rais Kalonzo Musyoka, ni mojawapo ya vyama vilivyo na nafasi bora ya kushinda kwenye uchaguzi mkuu ujao nchini Kenya.
Hata hivyo, muungano huo unaovishirikisha vyama mbalimbali vikiwemo Orange Democratic Movement (ODM), Wiper Democratic Party na chama cha FORD Kenya, unakabiliwa na ushindani mkubwa kutoka kwa muuungano wa mrengo wa Jubilee, unaongozwa na Naibu Waziri Mkuu Uhuru Kenyatta na mgombea mwenza William Ruto.
CORD wanaamini kuwa wako katika nafasi nzuri ya kutetea haki za Wakenya huku wakisisitiza kuwa sera za ilani yao zinalenga katika kukuza na kuimarisha uchumi wa nchi. Wanasiasa wa mrengo huo pia wanaligusia swala tete la ardhi. Wanasema wanadhamiria kutumia vipengee vya katiba mpya kuleta haki katika ugawaji wa ardhi.
Suala la ardhi la Kenya
Odinga na wenzake wanamkashifu mpinzani wao wa karibu Bw. Kenyatta wakidai kuwa hana haki kugombea uongozi wa nchi wakati familia yake na pia yeye binafsi wanamiliki mashamba makubwa makubwa bila ya kuwajali raia wengi nchini wasio na makao. Inadaiwa kuwa familia ya Bw.Kenyatta inamiliki sehemu kubwa ya ardhi, tena katika maeneo mengi nchini Kenya. Bw Musyoka anawakosoa wale wanaodai kuwa serekali yao itawalenga baadhi ya wamiliki wa mashamba. “wananchi wasiwe na wasiwasi kwani hapana yeyote atakaye nyang'anywa shamba lake analo limiliki kihalali, lakini tutahakikisha kuwa mashamba yamegawa na kustawishwa kwa njia ya haki. Alisema Musyoka”.
Bw. Odinga anasema nae akitilia mkazo jambo hilo kwa kusema “Hili ni jambo la kuvunja moyo kuwa kunao wakenya wanagombania vipande vidogo vidogo vya ardhi ilhali kunao wengine wenye kumiliki karibu mkoa mzima”. Hata hivyo, Bw. Kenyatta anakanusha madai hayo akisema kuwa hakuna kesi ye yote iliyowahi kuwasilishwa kortini dhidi yake juu ya swala la ardhi.
Muelekeo wa Elimu ya Kenya
Kuhusu maswala ya elimu, viongozi wa mrengo wa CORD wanaahidi kuwaajiri waalimu zaidi ili kufanikisha sekta hiyo muhimu.
Aidha, serikali ya Bw. Odinga inakusudia kuimarisha na kustawisha sekta ya kilimo na ufugaji kwa lengo la kuangamiza janga la njaa na kukidhi mahitaji ya chakula nchini. Kufanya hivyo, alisema serikali yake itajenga viwanda vya kuzalisha mbolea kama njia mojawapo ya kuwapunguzia gharama wakulima.
Akizungumza punde tu baada ya kuzindua rasmi manifesto hiyo, Bw. Odinga alitetea sera za mrengo wa CORD na kutoa ahadi kwamba serikali yake itafanya kila juhudi kuukwamua uchumi wa nchi na hivyo basi kuboresha hali ya maisha miongoni mwa wakenya wote kwa ujumla.
Mambo mengine mengi muhimu yanayoorodheshwa katika ilani ya CORD ni pamoja na ahadi ya kuilinda katiba mpya, kuimarisha huduma za afya miongoni mwa wakenya na pia kubana matumizi ya fedha za serikali.
Mwandishi: Rubein Kyama
Mhariri: Josephat Charo