Umwagaji damu waendelea Syria
29 Oktoba 2011Wanaharakati na wakaazi wamesema, waandamanaji kadhaa wamejeruhiwa na mamia wengine wamekamatwa katika umwagaji damu huo mkubwa kabisa, kwenye maandamano yanayoendelea nchini humo, tangu miezi saba, kudai mwisho wa utawala wa miaka 41 wa familia ya Assad.
Kufuatia umwagaji huo wa damu, mawaziri wa nchi za Kiarabu wametuma ujumbe mkali kabisa kwa Rais Assad wakimtaka asitishe mauaji ya raia. Kamati maalum ya Umoja wa Nchi za Kiarabu kuhusu mzozo wa Syria imesema, imepeleka risala ya dharura kwa serikali ya Syria kulalamika kuhusu mauaji ya raia wa Syria yanayoendelea nchini humo.
Kamati hiyo, katika taarifa iliyotolewa imesema, ni matumaini yake kuwa serikali ya Syria itachukua hatua kuwalinda raia. Mawaziri wa nchi za Kiarabu wamepanga kukutana na maafisa wa Syria katika mji mkuu wa Qatar, Doha, kesho Jumapili.
Mauaji ya siku ya Ijumaa hasa yalitokea katika miji ya Homs na Hama iliyo kati kati ya nchi. Miezi mitatu iliyopita Rais Assad alipeleka wanajeshi na vifaru katika mji wa Hama kuzima maandamano makubwa. Mji wa Homs ni kitovu cha upinzani unaozidi dhidi ya utawala wa mabavu wa Assad.
Baraza la Taifa la Upinzani la Syria limetoa mwito kwa jumuiya ya kimataifa kuwalinda raia. Baraza hilo halikuomba kuivamia kijeshi Syria lakini waandamanaji barabarani wanazidi kupaza sauti kudai hilo.