1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaAsia

Taliban kutangaza serikali karibuni, wataka kutambuliwa

Iddi Ssessanga
6 Septemba 2021

"Maamuzi ya mwisho yamechukuliwa na sasa tunashughulikia masuala ya kitaalamu," amesema msemaji wa Taliban Zabihullah Mujahid baada ya kutangaza ushindi katika mapigano ya kuwania mkoa wa mwisho wa bonde la Panjshir.

https://p.dw.com/p/3zzcj
Taliban Sprecher Zabihullah Mujahid
Picha: Hoshang Hashimi/AFP/Getty Images

Taliban imesema serikali mpya ya Afghanistan itakayotangazwa muda wowote inaweza kuwa "serikali ya mpito", kwa mtazamano kuelekea mabadilko huko mbeleni, wakati ikitangaza ushindi katika mkoa wa kaskazini wa bonde la Panjshir.

Wiki tatu baada ya kutwaa madaraka lakini kukiwa hakuna serikali iliyotangazwa mpaka sasa, msemaji wa Taliban Zabihullah Mujahid amesema mfumo wa serikali ya mpito utatangazwa kwanza ili kuruhusu mabadiliko.

Soma pia: Taliban yatangaza ushindi mkoa wa Panjshir

''Maamuzi yote na hatua za mwisho vimechukuliwa, na sasa tunashughulikia tu masuala ya kitaalamu ili kutangaza serikali," alisema wakati wa mkutano na wanahabari katika mji mkuu Kabul siku ya Jumatatu.

Afghanistan Kabul - Taliban PK
Msemaji wa Taliban Zabihullah Mujahid (katikati) akizungumza na vyombo vya habari kwenye uwanja wa ndege wa Kabul, Agosti 31, 2021, baada ya Marekani kuondoa wanajeshi wake wote.Picha: Wakil Kohsar/AFP/Getty Images

"Tutatangaza serikali mpya haraka baada ya masuala ya kitaalamu kutatuliwa."

Utambuzi wa kimataifa watafutwa

Mujahid amesema Taliban inatambua kwamba amani na utulivu ni vya lazima kwa ajili ya kuvutia uwekezaji, na kueleza matumaini ya kuwa na uhusiano mzuri na majirani wote wa taifa hilo, ikiwemo China.

Soma pia: Merkel asema jumuiya ya kimataifa lazima ikubali kuzungumza na kundi la Taliban

Ametoa wito kwa jumuiya ya kimataifa kungua tena balozi zao mjini Kabul, na kuongeza kuwa Afghanistan ina haki ya kutambuliwa.

"Vita vimeisha, nchi inaondoka kwenye mzozo. Ni wakati sasa kwa amani na ujenzi mpya. Tunahitaji watu kutuunga mkono." Alisema "Afghanistan ina haki ya kutambuliwa."

"Jumuiya ya kimataifa inapaswa kufungua balozi zao mjini Kabul," alisema.

Taliban wameripotiwa kuzialika Pakistan, Iran, Uturuki, China, Urusi na Qatar kuhudhuria hafla ya kutangaza serikali mpya.

Afghanistan Taliban Kämpfer in Kabul, Plakat "Islamisches Emirat Afghanistan"
Afghanistan sasa inajulikana kama Emarati ya Kiislamu ya Afghanistan.Picha: Bashir Darwish/UPI Photo/newscom/picture alliance

Uasi wowote mpya utasambaratishwa vibaya

Msemaji wa Taliban pia amewatolewa wito wanajeshi wa zamani wa jeshi la Afghanistan kujiunga na utawala mpya.

Soma pia: Taliban wazidi kufagia miji Afghanistan, dunia yashtushwa

"Vikosi vya Afghanistan vilivyopatiwa mafunzo katika miaka 20 iliyopita vitaombwa kujiunga tena na idara ya usalama sambamba na wanachama wa Taliban," Mujahid alisema.

Aliongeza kuwa uasi wowote dhidi ya utawala wao utasambaratishwa vibaya, baada ya kutangaza ushindi katika bonde la Panjshir.

"Emarati ya Kiislamu inaguswa sana kuhusu uasi. Yeyote anaejaribu kuanzisha uasi atapiga vibaya. Hatutaruhusu mwingine," alisema Mujahid.

"Yeyote atakaechukuwa silaha na kuanzisha uasi mwingine, bila shaka yoyote atauwa adui yetu."

Onyo hilo linajiri wakati kiongozi wa kundi la upinzani la National Resistance Front NFR, Ahmad Massoud, akiwatolea wito raia kuanza uasi wa umma dhidi ya Taliban, katika ujumbe wa sauti uliyotolewa leo Jumatatu, saa chache baada ya Taliban kutangaza ushindi dhidi ya kundi hilo.

Mapigano kati ya Taliban na NFR yalianza siku ya Jumanne iliyopita, baada ya majadiliano ya kufikia muafaka wa kisiasa kushindikana.

 Afghanistan | Taliban am Gouverneurssitz in Pandschir
Wapiganaji wa Taliban wakiwa mbele ya lango la kuingilia ofisi ya gavana wa jimbo la Panjshir, Septemba 6, 2021.Picha: Social media/REUTERS

Mujahid pia alisema wanawake wa Afghanistan hawapaswi kufanya maandamano kwa sababu ya hali "tete inayoendelea ya usalama", akisema maandamano ni haki "lakini wanapaswa kuwasiliana nasi."

Soma pia:Taliban kutangaza serikali mpya ya Afghanistan

Alisema pia kwamba mpiganaji wa Taliban ametiwa mbaroni kwa kukosa nidhamu na waandamanaji wa kike wiki iliyopita.

Kufunguliwa upya kwa uwanja wa ndege wa Kabul

Suala nyeti kwa Taliban ni mchakato unaoendelea wa kufunguliwa tena kwa uwanja wa ndege wa Kabul, ambako mpango mkubwa wa uondoaji ulioongozwa na Marekaniulikamilika wiki iliyopita.

Qatar imekuwa ikishirikiana na Taliban kuhusu kurejesha operesheni za uwanja huo na Majahid amesema "juhudi za kweli" zilikuwa zinaendelea kurejesha operesheni.

Soma pia: Kipi kinafuata Afghanistan baada ya kuibuka tena kwa Taliban?

"Timu za kiufundi kutoka Qatar, Uturuki na UAE zinafanyakazi kwa bidii kukarabati vifaa," alisema, na kuongeza kuwa safari za ndege za kimataifa zitarejea "haraka iwezekanavyo."

Siku za mwisho za vita vya Marekani vilivyodumu kwa miaka 20 nchini Afghanistan zilishuhudia uondoaji mkubwa katika uwanja wa ndege wa Kabul wa makumi ya maelf ya watu - Wamarekani na washirika wao - waliohofia mustakabali.

Operesheni kali ya Taliban iliyofagia kote nchini ilichukuwa chini ya moja tu kuvishinda vikosi karibu 300,000 vya jeshi la Afghanistan, ambao wengi wao walijisalimisha au kutoroka.

Soma pia: Maoni: Demokrasia ya Afghanistan imegeuka ya kadri

Majeshi ya Marekani yaliharibu kwa maksudi sehemu kubwa ya vifaa katika uwanja wa ndege wa Kabul kabla ya kuondoka, ikiwemo mifuno ya radar, na Mujahidi amesema itachukuwa muda kidogo kabla ya uwanja huo kurejea operesheni kikamilifu.

Chanzo: Mashirika