1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
UgaidiMali

Mali: Hatuna mpango wa kuzungumza na 'magaidi'

8 Mei 2026

Serikali ya Mali imetupilia mbali wazo la kuzungumza na makundi iliyoyataja kuwa ya kigaidi ambayo yanaendeleza uasi katika nchi hiyo ya Afrika Magharibi.

https://p.dw.com/p/5DUqa
Mali Bamako 2026 | Assimi Goïta akipiga saluti wakati wa shughuli ya mazishi ya Waziri wa Ulinzi Sadio Camara
Mali inapitia hali ya wasiwasi kutokana na mashambulizi ya waasiPicha: ORTM/REUTERS

Waziri wa Mambo ya Nje wa Mali Abdoulaye Diop amesema akizungumza na wanadiplomasia, kwamba serikali mjini Bamako haina mpango wowote wa kufanya mazungumzo na makundi ya kigaidi yanayoendesha shughuli zao kinyume cha sheria na ambayo yamehusika na matukio mabaya yaliyowakumba watu wa eneo hilo kwa miaka mingi.

Kauli ya waziri Diop imetolewa siku chache baada ya wapiganaji itikadi kali wa kundi la Ukombozi wa Azawad linalowajumuisha waasi wanaotaka kujitenga wa Touareg na washirika wao wa kundi la JNIM kuanzisha mashambulizi makubwa dhidi ya taasisi za uongozi wa kijeshi unaoiongoza Mali tangu mwaka 2020.

Mali Bamako 2026 | Mazishi ya kitaifa ya Waziri wa Ulinzi aliyeuawa Sadio Camara
Mali imekumbwa na hali ya wasiwasi hasa baada ya shambulizi la kigaidi lililotokea mjini Bamako Picha: ORTM/REUTERS

Watu zaidi wauawa kwenye mashambulizi

Alhamisi, vyanzo mbalimbali vililiambia shirika la habari la AFP kuwa mashambulizi mawili katikati mwa Mali yaliyofanywa na makundi hayo ya itikadi kali yenye mafungano na Al Qaeda yalisababisha vifo vya watu zaidi ya 30 katika vijiji vya Korikori na Gomossogou.

Kundi la waandishi wa habari waliobobea katika masuala ya usalama wa kanda ya Sahel wamesema idadi hiyo ya vifo inakadiriwakufikia watu 50 huku wengine wengi wakiwa hadi sasa hawajulikani walipo.

Kumeripotiwa pia msako unaoendelea dhidi ya wanasiasa wa upinzani na maafisa kadhaa wa kijeshi ambao wanaendelea pia kukamatwa na kushikiliwa na mamlaka za kijeshi. Waasi hao wamepata mafanikio kwa kuudhibiti mji wa Kidal na kambi muhimu ya kijeshi ya Tessalit huku wakizuia barabara nyingi zinazoelekea katika mji Mkuu Bamako.

Mali Bamako 2026 | Moshi mwingi umetanda mjini Bamako baada ya mashambulizi ya kupangwa yaliyofanywa na waasi
Jeshi la Mali limesema bado hali ya usalama ni tete nchini humo tangu baada ya shambulizi la waasiPicha: AFP

Jeshi: Hali ya usalama bado ni tete

Msemaji wa Jeshi la Mali Meja Djibril Maiga amesema zaidi ya maafisa 10,000 wa ndani na kutoka nje ya nchi wanashiriki zoezi la kuwadhibiti waasi hao lakini akasisitiza kuwa kuwa hali ya usalama bado ni tete. "Adui aliyekosa mwelekeo hakuwa na chaguo jingine, isipokuwa kuzuia barabara zinazoelekea mjini Bamako kwa kutumia mbinu tata."

Mamluki wa Urusi wa Africa Corps ambao zamani walijulikana kama Wagner wamesema wanaendelea kuisaidia serikali ya Mali kukabiliana na makundi hayo ambayo tayari yametangaza azma yao ya kuuangusha utawala wa kijeshi unaoongozwa na Jenerali Assimi Goita.