1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUfaransa

Sarkozy apoteza kesi ya rufaa juu ya ufisadi

Amina Mjahid
17 Mei 2023

Mahakama ya rufaa ya Ufaransa imetoa kifungo cha miaka 3 kwa rais wa zamani Nicolas Sarkozy kwa hatia ya ufisadi na kumshawishi jaji. Hatua hiyo imemnyima pia nafasi ya kushikilia nyadhifa umma kwa kipindi cha miaka 3.

https://p.dw.com/p/4RUaV
Frankreich | Bestechungs-Prozess gegen Ex-Präsident Sarkozy
Picha: Bertrand Guay/AFP/dpa/picture alliance

Mahakama ya rufaa imesema Nicolas Sarkozy rais wa zamani wa ufaransa anapaswa kutumikia kifungo cha nyumbani kwa mwaka mmoja, akivalia bangili ya kielektroniki na pia kumpiga marufuku ya kuwania nafasi yoyote katika ofisi za umma kwa miaka mitatu kufuatia kitendo chake cha kumshawishi jaji katika kesi dhidi yake.

Sarkozy aliye na miaka 68 aliondoka katika mahakama hiyo bila ya kutoa maoni yoyote juu ya uamuzi huo, lakini mawakili wake wamesema watakata rufaa kupinga uamuzi uliotolewa na mahakama hiyo ya juu ya rufaa nchini Ufaransa.

Sarkozy ahukumiwa kifungo cha mwaka mmoja jela

Sarkozy, aliyeiongoza Ufaransa kwa muhula mmoja kuanzia mwaka 2007 hadi 2012 amekuwa akiandamwa na matatizo ya kisheria tangu alipoondoka madarakani. Mwezi Machi mwaka 2021 alikuwa rais wa kwanza wa zamani wa Ufaransa, kuhukumiwa kwenda jela baada ya mahakama kumkuta na hatia ya kuwa yeye pamoja na wakili wake wa zamani Thierry Herzog walikubaliana kuhusu kutoa rushwa kwa jaji Gilbert Azibert ili kutoa au kuwapa taarifa kuhusu uchunguzi wa kisheria uliokuwa unaendelea.

Njama hiyo ilijulikana baada ya timu ya wachunguzi kuchunguza laini za simu mbili rasmi za Sarkozy na kugundua kuwa alikuwa pia na simu nyengine iyisorasmi iliyoacha kutumika mwaka 2014 iliyosajiliwa chini ya jina la "Paul Bismuth", na laini hiyo ya simu ndiyo iliyokuwa ikitumika kuwasiliana na Herzog. Mambo yaliyopatikana katika simu hizi ndio yaliyopelekea Sarkozy kufunguliwa mashitaka ya ufisadi aliyoyakana.

Rais Sarkozy aendelea kukanisha mashitaka dhidi yake

Frankreich | Nicolas Sarkozy
Rais wa zamani wa Ufaransa Nicolas Sarkozy Picha: Vincent Isore/IP3press/IMAGO

Sarkozy atafikishwa tena mahakamani Novemba mwaka 2023 katika kesi yake nyengine aliyoikatia rufaa inayojulikana kama kesi ya Bygmalion ambayo iliyomsababishia kupewa kifungo cha mwaka mmoja jela. Waendesha mashitaka walidai timu yake ilitumia mara mbili kiasi kinachokubalika katika kampeni yake ya mwaka 2012 na kutumia bili za kughushi katika kamouni ya mahusiano ya umma ya Bygmalion.

Katika kesi hiyo Sarkozy pia alikanusha kuhusika na sakata hilo. Pia anatazamiwa kushitakiwa kwa makosa mengine yanayodai Libya ilifadhili kampeni zake za mwaka 2007 wakati wa utawala wa Moammar Gaddafi.

Ufaransa: Rufani ya rais wa zamani Nicolas Sarkozy yatupwa

Sarkozy anatuhumiwa kwa makosa ya Ufisadi, ufadhili haramu wa kampeni zake na ubadhirifu wa mali ya umma lakini anakanusha madai yote hayo.  Licha ya matatizo yake mengi ya kisheria rais huyo wa zamani wa ufaransa, bado anaumaarufu na ushawishi nchini humo katika siasa za taifa hilo na anasikilizwa pia na rais wa sasa Emmanuel Macron.

Kabla ya Sarkozy, rais mwingine wa zamani wa Ufaransa ambaye alishitakiwa kwa makosa ya uhalifu, ni mtangulizi wake Jacques Chirac, aliyepewa kifungo cha miaka miwili mwaka 2011 kwa makosa ya ufisadi na sakata la ajira za uwongo iliyofungamanishwa na wakati wautawala wake alipokuwa meya wa Paris.

Chanzo: Reuters/AP/AFP