1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Papa Francis alaani "tamaa ya binaadamu"

Bruce Amani
25 Desemba 2018

Katika hotuba yake ya Mkesha wa Krismasi, kiongozi wa Kanisa Katoliki Ulimwenguni Papa Francis amesema, kwa watu wengi, maana ya uzima inapatikana katika umiliki wa mali nyingi kupindukia.

https://p.dw.com/p/3AbfH
Vatikan Papst kritisiert in Christmette menschliche Gier und Konsum
Picha: Reuters/M. Rossi

Misa ya Papa katika Mkesha wa Krismasi ndani ya Kanisa la Mtakatifu Petro mjini Vatican ni mojawapo ya sherehe muhimu zaidi za Kikatoliki kusherehekea kuzaliwa kwa Yesu Kristo.

Maelfu ya waumini walihudhuria misa hiyo ya Jumatatu usiku katika Kanisa la Mtakafitu Petro wakati Papa Francis mwenye umri wa miaka 82, kiongozi wa Wakatoliki bilioni 1.3 duniani, alitoa hotuba yake ya Krismasi.

Wageni kutoka kote ulimwenguni walimiminika mjini Bethlehem katika Mkesha wa Krismasi, kabla ya misa ya usiku wa manane, wakipanga mstari mrefu kuona eneo ambalo Yesu anaaminika kuzaliwa na kushiriki katika gwaride la sherehe.

Vatikan Papst kritisiert in Christmette menschliche Gier und Konsum
Francis alikumbusha kuwa Yesu alizaliwa katika umaskiniPicha: Reuters/M. Rossi

Bethlehem, mji ulio karibu na Jerusalem, lakini uliotenganishwa na kizuizi ilichoweka Israel, umeshuhudia ongezeko la wageni msimu huu baada ya miaka mingi ya kutoshuhudia wageni wengi kutokana machafuko yanayohusishwa na mgogoro kati ya Waisrael na Wapalestina.

Wakati huo huo, naibu wake ambaye ni Waziri wa Mambo ya Nchi za Kigeni, Pietro Parolin, aliongoza misa sanjari ya Mkesha wa Krismasi mjini Baghdad, katika ishara ya mshikamano na jamii ya Wakristo walio wachache nchini Iraq. Wakatoliki ni miongoni mwa jamii za walio wachache ambazo zinalengwa katika machafuko yanayochochewa na kundi linalojiita Dola la Kiislamu – IS ambapo maelfu ya watu wamekimbia makazi yao.

Parolin alikutana Jumatatu na Waziri Mkuu wa Iraq Adel Abdul-Mahdi. Anatarajiwa katika siku zijazo kuzuru kaskazini mwa Iraq kukutana na viongozi wa Kikurdi mjini Irbil na kusherehekea Misa katika eneo la Qaraqosh la Nineveh, karibu na Mosul, kwa mujibu wa Vatican.

Vatikan Papst kritisiert in Christmette menschliche Gier und Konsum
Karibu waumini 10,000 walihudhuria misa hiyoPicha: Reuters/M. Rossi

Papa Francis atatoa leo mchana ujumbe wake wa sita wa Urbi et Orbi tangu alipochukua wadhifa huo. Mara nyingi ujumbe wa UrbI et Orbi hutumiwa kuomba amani ulimwenguni na hutolewa wakati wa Siku Kuu ya Pasaka, Krismasi na baada ya kuchaguliwa Papa mpya.

Krismasi hii inaukamilisha mwaka ambao umekuwa mgumu kwa Papa Francis, ambapo Kanisa Katoliki likumbwa na mgogoro wa unyanyasaji wa watoto kingono na kuutia mashakani uwezo wa Papa kuushughulikia mgogoro huo

Katika hotuba yake ya Ijumaa, kiongozi huyo wa kanisa katoliki alirudia ahadi yake ya kuwakabili mapadre wanaofanya uovu huo.

Nchini Uingereza, Malkia Elizabeth II atatoa wito wa kuwepo na heshima katika ujumbe wake wa Krismasi huku nchi hiyo ikiwa imegawika pakubwa kuhusiana na mpango wake wa kujiondoa katika Umoja wa Ulaya.

Mwandishi: Bruce Amani/DPA/AFP