1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Papa Francis akemea usaliti Vatican

Sylvia Mwehozi
21 Desemba 2017

Kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani Papa Francis ametumia salamu zake za heri ya Christmas, akiwataka watendaji wa Vatican, kuwa waaminifu, kuepuka njama na makundi madogo.

https://p.dw.com/p/2pmL9
Vatikan Papst hält Weihnachtsansprache
Picha: Reuters/M. Rossi

Papa Francis ambaye anakabiliwa na upinzani mkali katika utawala wake na dhamira ya kuleta mageuzi ya kiroho, katika kipindi cha miaka iliyopita alitumia hotuba ya kila mwaka kukemea rushwa na matendo machafu ndani ya kuta za Vatican.

Mwanzoni mwa hotuba yake, Papa Francis amewaeleza makadinali, mapadre na maaskofu wanaofanya kazi naye kuwa "kuifanyia mageuzi Rome, ni sawa na kulisafisha sanamu la jiwe huko Misri kwa mswaki", akiongeza kwamba ni kazi inayohitaji uvumilivu, kujitolea na kwa uangalifu.

Katika hotuba yake aliyoitoa kwenye makaazi yake katika kanisa la mtakatifu Peter, Papa Francis amekiri kwamba kulikuwa na watu wengi wenye ujuzi, waaminifu na hata watakatifu ambao hufanya kazi katika maeneo matakatifu. Lakini akasema kuwa wapo wengine waliochaguliwa kufanyia mageuzi ufanisi mdogo wa Vatican na kuwaondoa watendaji ambao hawafai kwa ajili ya jukumu hilo.

Vatikan Papst hält Weihnachtsansprache
Papa Francis akiwasili kutoa hotuba ya mwaka Picha: Reuters/M. Rossi

Papa Francis ana utamaduni wakutoa ujumbe muhimu wa Christmas kwa kuwaalika watendaji wa vatican ambao wanamsaidia katika kazi ya kuongoza kanisa lenye waumini bilioni 1.2 kabla ya mwaka mpya. "Ni muhimu sana kuondokana na mantiki zisizo na usawa, zinazozalisha magenge na njama na hakika huwakilisha, licha ya utetezi wote na dhamira ya dhati, saratani zinazosababisha mitazamo ya kujitegemea, ambayo pia huingia katika kanisa na hususan watu wanaofanya kazi hapo."

Kauli hizo za Papa kupitia hotuba yake zinaonekana kama zinamlenga Libero Milone aliyekuwa mkaguzi mkuu ambaye alifutwa kazi mwezi Juni na baadae kudai kwamba jitihada zake za kusafisha mahesabu ya vatican, zilikuwa zinakwamishwa na "vigogo wa zamani" ambao wanafanya hivyo nyuma ya mgongo wa Papa.

Pia inaelezwa kuwa inawezekana ni ujumbe unaomlenga Kadinali wa Kijerumani Gerhard Lugwig Mueller ambaye mwezi Julai aliondolewa katika huduma ya mafundisho ya imani baada ya kumkosoa Francis kwa msimamo wake dhaifu juu ya masuala ya talaka.

Katika hotuba nyingine ya wafanyakazi wasio waumini, Francis ameomba msamaha akisema kuwa watumishi wa kanisa katoliki mara nyingi wamekuwa si watu wa mfano bora na pia akaahidi kuondokana na mikataba ya hatari Vatican. Tangu kuchaguliwa kwake kama Papa wa kwanza wa Amerika ya Kusini mwaka 2013, Francis amekuwa akijaribu kuleta mageuzi katika baraza kuu la watendaji wa kanisa katoliki linalotawaliwa kwa kiasi kikubwa na Italia ili kuleta uongozi wa kanisa karibu na wajumbe wake, kufanya mageuzi ya kiuchumi na kuliondoa katika kashfa za mtangulizi wake Papa Benedict.

Mwandishi: Sylvia Mwehozi/AP/dpa/reuters

Mhariri: Saumu Yusuf