1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaSudan

IOM: Karibu watu milioni 10.7 wakimbia makazi yao Sudan

27 Januari 2024

Karibu watu milioni 10.7 wameyakimbia makazi yao kutokana na mizozo nchini Sudan na milioni tisa miongoni mwao wakiwa ni wakimbizi wa ndani na wengine milioni 1.7 wakiwa wamekimbilia mataifa ya jirani.

https://p.dw.com/p/4bk5v
Vita vya Sudan | Wakimbizi wakiwa Chad
Wanawake waliokimbia vita nchini Sudan wakisubiri msaada wa kimataifa katika kambi ya Ourang karibu na mji wa Adre nchini ChandPicha: MOHANED BELAL/AFP

Taarifa ya karibuni zaidi ya Shirika la Kimataifa la Wahamiaji, IOM, imesema mzozo unaoendelea nchini Sudan kati ya jeshi la taifa, SAF na wanamgambo wa RSF umechochea idadi hiyo kubwa kabisa ulimwenguni ya watu walioyakimbia makazi yao.

Mkurugenzi wa IOM, Amy Pope amesema jana Ijumaa kwamba mmoja kati ya wakimbizi wanane wa ndani kote ulimwenguni ni wa nchini Sudan.

Amesema watu hao pia wanakabiliwa na upungufu mkubwa wa chakula, makazi na huduma za afya, lakini pia kitisho cha utapiamlo, magonjwa ya kuambukiza na machafuko.

Kulingana na shirika hilo, mzozo huo umeharibu miundombinu ya taifa, ikiwa ni pamoja na vituo vya afya, shule, barabara na vyanzo vya usambazaji wa nishati na maji pamoja na huduma za mawasiliano.