1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaAsia

Myanmar yakumbuka miaka miwili ya mapinduzi ya kijeshi

John Juma
1 Februari 2023

Maandamano ya kimya kimya yamefanyika kupitia migomo kote nchini Myanmar, huku wananchi wakikumbuka kupinduliwa kwa serikali iliyochaguliwa kidemokrasia na jeshi ambalo limeshika hatamu tangu tarehe 1 Februari 2021.

https://p.dw.com/p/4Mx5I
Thailand | Migranten aus Myanmar protestieren in Bangkok
Picha: Vachira Vachira/NurPhoto/picture alliance

Mitaa ilisalia mitupu na maduka kufungwa siku ya Jumanne (1 Februari) kama sehemu ya maandamano, mnamo wakati nchi hiyo inafanya kumbukumbu ya miaka miwili tangu mapinduzi ya kijeshi yaliyomuondoa madarakani kiongozi wa kiraia, Aung San Suu Kyi na serikali yake.

Haya yanajiri huku utawala wa kijeshi ukidokeza unaweza kurefusha hali ya hatari na kuchelewesha uchaguzi.

Myanmar imekuwa katika hali ya machafuko tangu mapinduzi hayo yaliyofuatiwa na ukandamizaji dhidi ya waandamanaji na kuchochea mapigano kote nchini humo na kudhoofisha uchumi.

Soma zaidi: Jeshi la Myanmar latuhumiwa kwa uhalifu wa kivita nchini Ujerumani

Myanmar yawaachia huru wafungwa 7,000 siku ya Uhuru

Nchi za Magharibi zimetangaza vikwazo vipya dhidi ya majenerali nchini Myanmar, lakini duru za awali za vikwazo zimeonesha dalili ndogo ya kuwashinikiza wanajeshi wa Myanmar kuachia madaraka.

Taarifa ya Wizara ya Fedha ya Marekani imeeleza kuwa nchi hiyo imeweka vikwazo vipya kwa Tume ya Uchaguzi, kampuni za biashara ya madini, maafisa wa kijeshi na wataalamu wa masuala ya nishati.

Canada, Australia na Uingereza nazo pia zimetangaza kuiwekea Myanmar vikwazo.