1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Muungano mpya wa siasa wazinduliwa nchini Kenya

Shisia Wasilwa3 Septemba 2021

Wanasiasa kadhaa akiwemo Spika wa Bunge Justin Muturi,wamejiunga katika walichokiita ''Muungano wa Wazalendo'' watakachokitumia kuwania kiti cha urais.

https://p.dw.com/p/3zrOU
Kenia Oppositionsführer Musalia Mudavadi, Raila Odinga, Isaac Ruto, Kalonzo Musyoka, and Moses Wetangula  in Nairobi
Picha: Reuters/T. Mukoya

Wakizungumza katika mji wa Wote katika jimbo la Makueni, viongozi hao watatu wameapa kushirikiana ili kushinda katika uchaguzi mkuu utakaoandaliwa tarehe tisa mwezi Agosti mwaka ujao. Spika Muturi aliwahimiza wakazi wa Makueni, kuunga mkono muungano huo mpya, akiwaahidi kuwa utashughulikia maslahi ya wakenya wa kawaida na kwamba watazunguka kwa wananchi kutafuta uungwaji mkono.

"Hatutaki kuambiwa na mtu mwingine kuwa nyinyi mtawekelewa mkono, hatutaki kuwekelewa mkono, hatutaki watu waketi mahali, kisha waseme nyinyi ndio tunawawekelea mkono, mkono ni wa mungu na Wakenya.” alisema Muturi.

''Tunataka tujichunge''

Muturi, Kituyi, Kibwana na Karua wamesema kuwa mlango wa muungano huo uko wazi kwa viongozi wengine wenye nia kama yao, lengo lao kuu likiwa kurithi kiti cha rais Kenyatta atakapokamilisha muhula wake wa mwisho. Karua alisema kuwa Kenya inahitaji mabadiliko mapya kutoka kwa kiongozi asiye na doa na kwamba wataendelea kufanya mikutano siku zijazo. 

"Tusipofikiria kama Kenya, ni nani atakuja kama rais? Kenya itaendelea kuumia, tunataka tujichunge na tuchunge kura zetu, tusiletewe viongozi ambao ni vifaranga vya kompyuta.”,alisema Karua.

Joto la uchaguzi mkuu wa 2022

Uchaguzi Mkuu Kenya umetarajiwa kuitishwa Agosti mwaka 2022 ambao Kenyatta hatowania tena.
Uchaguzi Mkuu Kenya umetarajiwa kuitishwa Agosti mwaka 2022 ambao Kenyatta hatowania tena.Picha: Reuters

Karua ni mmoja wa viongozi wa Muungano wa Chama Cha Kazi kinachowajumuisha mbunge wa Gatundu Moses Kuria na kiongozi wa Chama cha Huduma Mwangi Kiunjuri, waliouzindua Agosti tarehe 12 wakitaja kuwa muungano huo utapigia debe maslahi ya wakazi wa Mlima Kenya. Viongozi hao wameafikiana kufanya kongamano katika mji wa Limuru, katika kipindi cha miezi mitatu ijayo ili kufanya maamuzi ya utendajikazi wake. Mukhisa Kituyi ni mmoja wa viongozi hao, japo muungano huo haujataja nani atakayepeperusha bendera yake.

"Mimi niko tayari, kama inaonekana kuwa Kituyi ndiye atawaleta pamoja mimi nitamuunga mkono.” alisema Kituyi.

Wafuasi wa muungano mpya

Wakati huo huo, zaidi ya viongozi 40 kutoka maeneo ya wafugaji nchini Kenya, wametangaza kuunganisha jamii zao ili kuunga mkono, ushirikiano kati ya Rais Uhuru Kenyatta na kiongozi wa ODM Raila Odinga na kuzuia ushawishi wa Makamu wa Rais William Ruto katika maeneo hayo. Viongozi hao waliotoka katika majimbo ya Turkana, Samburu, Marsabit, Isiolo, Mandera, Garissa, Wajir, Tana River na Lamu, wamebuni vuguvugu kwa jina Upya litakalotumika kufikia malengo yao.