1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Miripuko yaitikisa Damascus, zaidi ya 53 wauawa

Admin.WagnerD21 Februari 2013

Miripuko isiyopungua minne ya mabomu imeutikisa mji wa Damascus, moja wapo karibu na makao makuu ya chama tawala nchini Syria cha Baath, na kuua watu wasiyopungua 53.

https://p.dw.com/p/17j7m
Magari yakiwaka moto kufuatia mripuko mbaya zaidi mjini Damascus tarehe 21.02.2013.
Magari yakiwaka moto kufuatia mripuko mbaya zaidi mjini Damascus tarehe 21.02.2013.Picha: Reuters

Watu wengine kadhaa wamejeruhiwa katika mashmabulio hayo ambayo pia yamepelekea uharibifu mkubwa wa miundombinu, wakati ambapo waasi wanasema wako tayari kuzungumza na serikali ya nchi hiyo.

Shirika la uangalizi wa haki za binaadamu nchini humo lenye makao yake mjini London Uingereza, lilisema hapo awali kuwa watu wasiyopungua 31 waliuawa katika mripuko huo, lakini taarifa iliyotolewa na Televisheni ya serikali muda mfupi uliopita inasema kuwa idadi ya waliokufa si chini ya watu 53 wengi. Televisheni ya Al-Akhbariya inayounga mkono utawala wa Assad iliyonyesha miili ya watu walioungua ikiwa imelala karibu na magari yanayowaka moto, na kusema kuwa watoto walikuwa miongoni mwa waliojeruhiwa kwa sababu mripuko huo ulitokea karibu na shule.

Moshi mweusi ukitanda katika anga ya mji wa Damascus kufuatia mripuko wa bomu lililouwa watu zaidi ya 53 tarehe 21.02.2013.
Moshi mweusi ukitanda katika anga ya mji wa Damascus kufuatia mripuko wa bomu lililouwa watu zaidi ya 53 tarehe 21.02.2013.Picha: picture alliance / dpa

Muda mfupi baada ya mripuko huo wa asubuhi, maroketi mawili yalirushwa dhidi ya makao ya jeshi mjini Damascus, iliripoti Al-Alkhbariya pamoja na shirika hilo la uangalizi wa haki za binaadamu bila kutoa taarifa zaidi kuhusu waathirika. Bomu la kwenye gari liliripuka katika uwanja wa 16 Novemba, karibu na msikiti wa AL-Imam, karibu na makao makuu ya chama cha Baath kilichoitawala Syria kwa nusu karne sasa. Majengo yaliharibiwa vibaya katika shambulio, na kupelekea moshi mzito kutanda katika anga ya Damascus.

Muungano wa Taifa wa Syria walaani

Hakuna aliyedai kuhusika na shambulio hilo lalkini kundi la wapiganaji la Al-Nusura Front limedai kuhusika na mashambulizi mengi ya kujitoa mhanga katika miezi ya hivi karibuni. Muungano wa upinzani wa umelaani shambulio hilo na kusema katika ukurasa wake wa facebook kuwa vitenmdo vyovyote vinavyowalenga raia kwa mauaji au ukiukaji wa haki zao ni uhalifu na vinafaa kulaaniwa.

Mashirika ya habari ya Urusi yaliripoti kuwa madirisha ya ubalozi wa nchi hiyo mjini Damascus yalivunjwa na kishindo cha mripuko huo, lakini hakuna kati ya wafanyakazi w aubalozi huo aliyejeruhiwa. Urusi ni moja ya mataifa makubwa machache yanayoendeleza uhusiano na utawala wa rais Bashar al-Assad wakati wa mgogoro na waasi na imeendeleza uwepo wake wa kidiplomasia mjini Damascus.

Watu wakipita karibu na magari yaliyoharibiwa na mripuko huo.
Watu wakipita karibu na magari yaliyoharibiwa na mripuko huo.Picha: Reuters

Huku hayo yakijiri, taarifa nyingine zinasema ndege za serikali zimefanya mashambuli zi dhidi ya hospitali moja katika mji wa kusini wa Daraa na kuua watu wasiyopungua 18 wakiwemo waasi wanane, wahudumu watatu wa afya, na raia saba, limesema shirika la uangalizi wa haki za binaadamu ambalo linakusanya taarifa zake kutoka kwa mtandao wa wanaharakati walioko ndani ya Syria.

Mazungumzo sawa lakini bila Assad

Naye waziri wa mambo ya kigeni wa Uingereza William Hague, ameushauri utawala wa rais Bashar Al-Assad kuitikia vyema kwa pendekezo la majadiliano lilitolewa na mkuu wa upinzani Ahmed Moaz al-Khatib. Waziri Hague pia alimtaka Assad kuachia madaraka mwenyewe, akisema watu wa Syria wameteseka vya kutosha.

Muungano wa upinzani umetoa taarifa kuwa uko tayari kuzungumza amani chini ya usimamizi wa Urusi na Marekani, lakini ukasisitiza kuwa Rais Assad hawezi kuwa sehemu ya mazungumzo hayo.

Mwandishi: Iddi Ismail Ssessanga/rtre, afpe, dpa, afp
Mhariri: Saum Yusuf