1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mawaziri 3 Kenya wadaiwa kuwa na njama ya kumuua naibu rais

Shisia Wasilwa, Nairobi24 Juni 2019

Mawaziri watatu wa Kenya Peter Munya, Cecilly Kariuki na Joe Mucheru wamehojiwa katika makao makuu ya upelelezi jNairobi, kuhusiana na madai ya kupanga njama ya kumuua naibu wa rais William Ruto.

https://p.dw.com/p/3KzdJ
Mawaziri Peter Munya, Sicily Kariuki na Joe Mucheru wakitoka kuandikisha taarifa kwenye ofisi za upelelezi Nairobi Kenya.
Mawaziri Peter Munya, Sicily Kariuki na Joe Mucheru wakitoka kuandikisha taarifa kwenye ofisi za upelelezi Nairobi Kenya.Picha: DW/S. Wasilwa

Mawaziri watatu nchini Kenya, wamekanusha madai ya kupanga njama ya kumuua naibu rais William Ruto ili kuzuia azma yake ya kuwania kiti cha urais katika uchaguzi mkuu ujao. Hata hivyo mawaziri hao wamekataa kuandikisha taarifa wakisema kuwa, naibu rais mwenyewe hajawasilisha malalamiko rasmi katika kituo cha polisi. Ruto ndiye mwanasiasa mkuu ambaye anatazamiwa kumrithi rais Kenyatta pindi atakapokamilisha utawala wake.

Watatu hao waliohojiwa katika makao makuu ya upelelezi walikuwa waziri wa Viwanda, Peter Munya, waziri wa Afya Cecilly Kariuki na wa Teknolojia na Mawasiliano Joe Mucheru. Akizungumza na wanahabari kwa niaba yao, Peter Munya alisema kuwa madai hayo hayana msingi wowote na kukiri kuwepo kwa mikutano ambayo imekuwa ikifanyika kuhusu maendeleo ya eneo la Mlima Kenya anakotokea rais Kenyatta.

"Kitu cha kwanza hakuna malalamishi yoyote ambayo yameandikishwa kwenye kitabu cha matukio, ambayo tunaweza kuyajibu hata kama tungetaka hakuna mlalamishi.”

Mawaziri 3 wa kenya wadaiwa kupanga njama ya kutaka kumuua naibu rais William Ruto.
Mawaziri 3 wa Kenya wadaiwa kupanga njama ya kutaka kumuua naibu rais William Ruto.Picha: DW/S. Wasilwa

Munya alisema kuwa mkurugenzi wa Upelelezi wa visa vya jinai aliwataka wafike katika makao makuu ya uplelezii, baada ya Naibu rais William Ruto kulalamika kupitia mawasiliano kwa njia ya simu. Watu hao wanne hao wamesema kuwa wana uhuru wa mahusiano na kwamba mkutano wao umetokana na ukweli kuwa eneo hilo limetengwa kwenye masuala ya maendeleo. Gavana huyo wa zamani wa jimbo la Meru pia alisema kuwa rais Uhuru Kenyatta alimpa jukumu la kuandaa mikutano kati ya viongozi na maafisa wa serikali kutafuta suluhisho kwa matatizo ya wakazi wa Mlima Kenya.

"Bila shaka haya ni madai mazito, hasa yanapotoka kwa mtu wa hadhi na ofisi ya naibu rais. Nilitarajia mtu wa hadhi hiyo, kufanya uchaguzi wa kina, kabla ya kukurupuka na madai hayo. Nadhani ni ukosefu wa uwajibikaji.” Munya amesema.

Kwa mujibu wa mawaziri hao wanaotokea Mlima Kenya, ni kwamba Naibu rais Ruto, anadai kuwa baadhi ya maafisa serikalini kutoka eneo hilo walikuwa wanafanya mikutano ya siri ya jinsi ya kumuua. Njama hizo kwa mujibu wa Ruto ni za kumzuwia kutowania kiti cha urais baada ya Kenyatta kumaliza mihula yake. Katika baraza la mawaziri ambalo hufanyika kila juma Ruto hajawahi kuibua madai hayo.

"Watu wengi wanasumbuka ati mimi natembea Kenya hii. Wanataka niende wapi na siku ya kwenda mbinguni haijafika. Hata kuenda mbinguni nimejipanga pia. Kwa sababu Yesu hajarudi mim nitatembea Kenya hii.” Amesema William Ruto.

Matukio haya ni ishara kuwa chombo cha Jubilee kinazidi kuzama kwenye bahari, kama kitaibuka baada ya misukosuko hii, ni suala jingine