1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mapigano makali yasababisha mauaji ya watu 20, Afar Ethiopia

Amina Mjahid
22 Julai 2021

Maafisa nchini Ethiopia wasema watu 20 wameuwawa na wengine wengi wamepoteza makaazi yao kufuatia mapigano makali kati ya waasi na vikosi vya serikali, katika eneo la Afar karibu na jimbo linalokumbwa na vita la Tigray

https://p.dw.com/p/3xtVA
Äthiopien I Situation in Tigray
Picha: Ben Curtis/AP/picture alliance

Kulingana na Umoja wa Mataifa, mapigano hayo katika eneo la Afar, yanaongeza hatari ya mzozo wa miezi minane wa Ethiopia kupanuka zaidi kushinda hali ilivyokuwa katika jimbo la Tigray ambako maelfu ya watu wameuwawa na wengine wengi kukabiliwa na njaa.

Waasi wa Tigray mwishoni mwa Juma walitekeleza kile msemaji wao alichokiita hatua ndogo katika jimbo la Afar wakiwalenga wanajeshi na wapiganaji kutoka jimbo la Oromia.

soma zaidi: Mzozo wa Tigray unaweza kuchochea vurugu za kikabila

Lakini Mohammed Hussen, afisa mmoja kutoka kwa shirika la kushughulikia majanga ya kitaifa lililoko Afar, ameliambia shirika la habari la AFP kwamba mashambulizi yalikuwa makubwa na raia walilengwa pia katika mashambulizi hayo.

Amesema mapigano hayo bado yanaendelea na watu takriban 70,000 wameathirika moja kwa moja huku akithibitisha kuuwawa raia 20 katika jimbo hilo.

Licha ya Abiy kutangaza ushindi bado mapigado yanaendelea

Äthiopien Premierminister Abiy Ahmed
Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy AhmedPicha: Tiksa Negeri/REUTERS

Waziri Mkuu wa Ethiopia, Abiy Ahmed alituma wanajeshi wake katika jimbo la Tigray mwezi Novemba mwaka jana kukitokomeza chama cha Ukombozi wa Watu wa Tigray, TPLF kinachotawala katika eneo hilo hatua anayosema ameichukua kutokana na waasi wa TPLF kushambulia makambi ya wanajeshi wa serikali kuu.

Licha ya Abiy mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel alitangaza ushindi mwezi uliopita katika vita hivyo, kiongozi wa TPLF bado hajulikani aliko na vita bado vinaendelea katika eneo hilo.

Mwezi uliopita vita hivyo vilichukua mkondo tofauti wakati wapiganaji wa TPLF walipoudhibiti tena mji mkuu wa jimbo la Tigray, Mekele na Abiy kutangaza pande zote kukubaliana kusitisha mapigano.

Lakini licha ya hayo yote mapigano yanaendelea hasa magharibi na kusini mwa Tigray. Mapigano katika jimbo la Afar tayari yamesambaratisha juhudi za kupeleka misaada katika jimbo linalokumbwa na vita la Tigray.

Msafara wa magari kutoka kwa shirika la mpango wa chakula duniani WFP, ulishambuliwa Afar hatua iliyolilazimisha shirika la Umoja wa Mataifa kusitisha safari ya magari yake ya misaada yaliyokuwa yaondoke kutoka mji wa Samera.

 Chanzo: afp, dpa