1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Joseph Kabila ahukumiwa kifo kwa uhaini

1 Oktoba 2025

Mahakama ya kijeshi nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo imemhukumu kifo aliyekuwa rais wa nchi hiyo Joseph Kabila baada ya kumtia hatiani kwa makosa kadhaa makubwa yakiwemo uhaini, uasi na uhalifu dhidi ya ubinadamu.

https://p.dw.com/p/51JBb
Marekani New York 2018 | Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo - Joseph Kabila akizungumza kwenye Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa Sept. 26, 2018
Rais wa zamani wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo Joseph Kabila akizungumza kwenye Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa Sept. 26, 2018Picha: Qin Lang/Photoshot/picture alliance

Hukumu hiyo imetolewa jana Jumanne na Luteni Jenerali Joseph Mutombo Katalayi mjini Kinshasa bila ya yeye mwenyewe kuwepo.

Kabila alipatikana na hatia ya kushirikiana na kundi la waasi la M23 linaloipinga serikali, na ambalo limeteka maeneo mengi ya mashariki mwa Kongo yenye utajiri mkubwa wa rasilimali wakisaidiwa na Rwanda.

Aliondoka nchini humo mwaka 2023 na kuonekana tena mwezi Mei mwaka huu katika mji wa Goma unaokaliwa na waasi hao hatua iliyoibua  wasiwasi mjini Kinshasa.

Wafuatiliaji wa mambo wanasema hukumu hiyo inalenga tu kuzuia azma yake ya kuunganisha upinzani, licha ya kwamba hajulikani aliko kwa sasa.