Idadi ya tembo Kenya yaongezeka katika miongo mitatu
14 Agosti 2020Shirika la huduma ya wanyapori nchini Kenya, KWS, lilitangaza siku ya Jumatano kuwa juhudi za kudhibiti ujangili zimesaidia idadi ya tembo nchini Kenya kuongezeka mara mbili katika miongo mitatu iliyopita.
Mkurugenzi wa KWS, John Waweru, alisema wakati wa ziara yake katika hifadhi ya wanyamapori ya Amboseli katika kuadhimisha siku ya tembo duniani, kulikuwa na tembo 16,000 tu nchini Kenya mnamo mwaka 1989, lakini ilipofika mwaka 2018 idadi hiyo iliongezeka zaidi ya tembo 34,000.
Waziri wa Utalii nchini Kenya, Najib Balala, akizungumza wakati wa maadhimisho hayo, alisema kuwa kwa miaka kadhaa iliyopita, Kenya ilifanikiwa kudhibiti vitendo vya ujangili nchini humo.
Soma pia Kenya yateketeza marundo ya pembe za tembo
Kama sehemu ya maadhimisho hayo, waziri wa utalii Najib Balala alisaidia kuchonga tembo mkubwa na akatoa jozi ya ndama mapacha na kusema "leo pia tunazindua kampeni ya kumtaja tembo wa kichawi wa Kenya, tamasha la kila mwaka ambalo lengo lake litakuwa ni kukusanya pesa lililotajwa kusaidia ustawi wa askari wanyamapori."
Balala alikuwa akimaanisha walinzi wenye silaha wenye jukumu la kuzuia majangili, na kuongeza kuwa mwaka huu pekee takribani ndama tembo 170 wamezaliwa.
Ujangili washuka pakubwa 2020
Idadi ya tembo waliouwawa na majangili nchini Kenya mnamo mwaka 2020 imeshuka kwa kiasi kikubwa kutoka miaka iliyopita ni tembo saba tu waliouwawa hadi hivi sasa mwaka huu ikilinganishwa na tembo 34 mnamo mwaka 2019 na tembo 80 mnamo mwaka 2018.
Barani Afrika kwa ujumla, takwimu zinaelezea hadithi mchanganyiko. Ujangili umeathiri vibaya idadi ya tembo kwa miongo kadhaa. Afrika ilikuwa ndio nyumbani kwa tembo milioni 1.3 katika miaka ya 1970, lakini kwa sasa ina tembo takribani 500,000 tu. Tembo chini ya 30,000 ndio wanakadiriwa kubaki porini.
Soma pia Twiga katika hatari ya kutoweka
Kenya na nchi nyingine za kusini mwa jangwa la Sahara katika miaka ya hivi karibuni zimeshuhudia kuongezeka kwa matukio ya ujangili, unaosababishwa na mahitaji ya pembe za ndovu na faru katika bara la Asia ambazo hutumiwa katika dawa za kitamaduni.
Serikali ya Kenya imetangaza hadharani jitihada zake za kudhibiti ujangili. Mnamo mwaka 2016 rais wa nchi hiyo Uhuru Kenyatta alichoma moto shehena ya pembe za ndovu na faru kutuma ujumbe kwa majangili na wanaofanya ulanguzi.
Soma pia Afrika yaungana katika vita dhidi ya kuangamia kwa tembo
Serikali pia imeanzisha adhabu kali ya faini na vifungo vikubwa jela kwa kila mtu anatiwa hatiani kwa ujangili wa wanyamapori au usafirishaji wa nyara za wanyamapori.
Chanzo: DW