1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

FC Kolon iko njia panda hadi sasa ina pointi mbili

Sekione Kitojo
23 Oktoba 2017

FC Kolon  iko  njia  panda , mashabiki  wajiuliza  ndio  safari ya daraja  la  pili ?  Bayern Munich sasa  pointi  sawa  na  Borussia Dortmund , ligi  ya  Ujerumani  Bundesliga  yazidi kupamba  moto.

https://p.dw.com/p/2mMcM
1. Bundesliga 9. Spieltag |  1. FC Köln - Werder Bremen
Picha: Getty Images/Bongarts/D. Mouhtaropoulos

Hoffenheim  walilazimika  kukubali  sare  ya  bao 1-1 dhidi  ya Wolfsburg  wakati  FC Kolon  na  Werder  Bremen  zimeendelea kubakia  bila  ushindi  katika  msimu  huu  wa  Bundesliga  baada  ya kutoka  sare  jana  bila  kufungana. FC Kolon  ambayo  inashika mkia  katika  msimamo  wa  ligi  imepata  pointi  yake  ya  pili  msimu huu  baada  ya  michezo  tisa. Kocha  wa FC Kolon Peter Stoger amesema  ilikuwa  bahati  mbaya kwamba  kikosi  chake hakikuzawadiwa pointi  tatu  muhimu.

1. Bundesliga 9. Spieltag |  1. FC Köln - Werder Bremen
Mchezaji mkongwe wa FC Koln Claudio Pizaro akishangaa mchezaji wa timu yake alivyokosa baoPicha: picture-alliance/augenklick/firo Sportphoto/C. Kaspar-Bartke

"Yalikuwa  mapambano  makali.  Mipango  katika  mchezo  huu haikuwa  kama  tulivyoipanga , ama  kama  vile  timu  inapokuwa katika  hali  hii  inavyotakiwa  kucheza, na  kutokana  na  hali  ilivyo haikuwa  mbaya sana.

Nafikiri , timu  zote  mbili zilichukua  hatua zote zinazostahili. Kulikuwa  na  nafasi  nyingi  za  kufunga  mabao , na kushinda  mchezo  huo. Kwa  matokeo  haya,  hakuna  kati  yetu anayeweza  kwa usahihi  kuanzisha  kitu. Ndio  sababu  tathmini yangu  kuhusu  mchezo  huu ni  kwamba  nilichokitaka , vijana  wangu wamekifanya. Kumekuwapo  na  hamasa  kubwa  katika  mchezo huu bila  shaka."

Fußball Augsburg Deutschland 09 09 2017 1 Bundesliga 3 Spieltag FC Augsburg 1 FC Köln Trainer Stöger
Kocha wa FC Koln Peter StoegerPicha: Imago/DeFodi/P. Fastl

Kocha  wa  Bremen Alexander Nouri  amesema  kikosi  chake kilipoteza  udhibiti  wa  mipira  mara  kwa  mara  na  kwamba  hiyo  ni sehemu  mijawapo  ambayo  wachezaji  wake  wanapaswa  kufanyia kazi.

Hoffenheim iko katika njia salama

Licha  ya  sare  ya  bao  1-1 Hoffenheim  ilipanda  na  kujiweka katika  nafasi  ya  nne  ya  msimamo  wa  ligi , huku  Bayern Munich baada  ya  ushindi  mwembamba  wa  bao 1-0 dhidi  ya  Hamburg SV ambayo  ilicheza  kwa  kipindi  kirefu  cha  mchezo  huo ikiwa  na wachezaji  10  uwanjani imefikisha  pointi 20  sawa  na  Borussia Dortmund  ambayo  katika  muda  wa  wiki  mbili  zilizopita imekuwa ikisuasua  na  kuonesha  udhaifu  katika  safu  yake  ya  ulinzi.

1. Bundesliga 9. Spieltag | VfL Wolfsburg - TSG Hoffenheim | TOR Elfmeter Hoffenheim
Wachezaji wa Hoffenheim wakishangiria bao Picha: Getty Images/AFP/J. MacDougall

Dortmund  ilitoka  sare  ya  mabao 2-2  na  Eintracht  Frankfurt baada  ya  kuongoza  kwa  mabao 2-0. Huyu  hapa  mshambuliaji  wa pembeni  wa  Borussia  Dortmund  Maxmillian Philipp.

"Tumefadhaika  mno , na  hii  inaweza  kuonekana  katika  nyuso zetu. Tulifanya kazi  kubwa. Tulijua  kuwa  Frankfurt  ni  timu  nzuri, ambayo  inaonesha  uwezo  mkubwa. Na  leo  wamefanya  hivyo. Sijui , iwapo  tulidhani kila  kitu  kimemalizika. Kwa  kuongoza  kwa mabao 2-0 hili halikupaswa  kutokea, katika  muda  wa  dakika  tano tunafungwa  mabao 2, inaumiza."

RB Leipzig  ni  ya  tatu baada  ya  kuishinda  Stuttgart  kwa  bao 1-0.

Leverkusen yacharuka

Bayer Leverkusen  iliirarua  Borussia  Moenchengladbach  kwa mabao 5-1  na  kujiimarisha  zaidi  katika  msimamo  wa  ligi  ambapo hivi  sasa  iko  nafasi  ya  tisa  ikiwa  na  pointi  12 nyuma ya Gladbach  ambayo  ina pointi 14  ikiwa  katika  nafasi  ya  8.

Michuano  ya  kombe  la  shirikisho  nchini  Ujerumani  DFB Pokal duru  ya  pili  inarejea  uwanjani  kesho  Jumanne  na  Jumatano , ambapo michuano  muhimu  ni  inatarajiwa  kuwa  siku  ya Jumatano, ambapo RB Leipzig  inaikaribisha  Bayern  Munich na Bremen  ikipambana  na  Hoffenheim.

1.Bundesliga 9. Spieltag | RB Leipzig - VfB Stuttgart
Kikosi hatari cha vijana wa RB Leipzig Picha: Getty Images/Bongarts/M. Kern

Pambano  la  RB Peipzig  na Bayern  Munich  linavuta  hisia  za  mashabiki  wa  soka  hapa Ujerumani  baada  ya  Bayern  kumrejesha  kocha  wake  wa  zamani Jupp  Heynckes  kukinoa  kikosi  hicho  ambacho  kilikuwa kikinolewa  na  kocha  Mtaliani  Carlo  Anchelotti.

Bayern  Munich haijapata  changamoto  kubwa  kutoka  kwa  vijana  hao  wa  Leipzig tangu  waingia  katika  ligi  daraja  la  kwanza  msimu  uliopita. Katika ligi  Leipzig  haija fua  dafu  mbele  ya  miamba  hao  kutoka  Munich, ambapo katika  mchezo  wa  kwanza  walibugia  mabao 3-1  na mchezo  wa  pili  Bayern  Munich  ilishinda  kwa  mabao 5-4.

Hivyo  macho  yote  yatakodolewa  siku  ya  Jumatano  katika mchezo  huo ambapo  vijana  wa  Leipzig  wakiwa  nyumbani wanatarajia  makubwa.

1. Bundesliga 9. Spieltag | Eintracht Frankfurt - Borussia Dortmund | TOR Dortmund
Wachezaji wa Borussia DortmundPicha: Reuters/K. Pfaffenbach

Ikiwa  wataitoa Bayern  katika  DFB Pokal itakuwa  ni  mara  ya kwanza  Bayern  kuaga  mashindano  haya  katika  duru  ya  pili.

Kesho Jumanne Borussia  Dortmund  inapambana  na  Magdeburg timu  ya  daraja  la  tatu , wakati  Schalke 04  inakwaana  na  Wehen Wiesbaden  pia  ya  daraja  la  tatu. Leverkusen  inapambana  na Union Berlin  na  Mainz inakwaana  na  Kiel  iliyoko  daraja  la  pili.

 

Mwandishi: Sekione  Kitojo / rtre / afpe / dpae

Mhariri:  Mohammed Abdul rahman