1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Eritrea yasema wanajeshi wake wako Tigray, yaapa kuwaondoa

Bruce Amani
17 Aprili 2021

Eritrea imekiri kwa mara ya kwanza kwamba wanajeshi wake wanashiriki katika vita vya mkoa wa kaskazini mwa Ethiopia wa Tigray lakini imetoa hakikisho la kuwaondoa baada ya kuongezeka kwa shinikizo la kimataifa

https://p.dw.com/p/3sANc
Bildergalerie Äthiopien | Flucht aus der Region Tigray
Picha: Baz Ratner/REUTERS

Eritrea imekiri kwa mara ya kwanza kwamba wanajeshi wake wanashiriki katika vita vya mkoa wa kaskazini mwa Ethiopia wa Tigray lakini imetoa hakikisho la kuwaondoa baada ya kuongezeka kwa shinikizo la kimataifa.

Soma pia: Eritrea inatakiwa kuviondoa vikosi vyake Ethiopia

Hatua ya mwanzo ya kukubali kwa uwazi kabisa kwa jukumu la Eritrea katika mapigano hayo imewekwa wazi katika barua iliyosambazwa katika mtandao Ijumaa na waziri wa habari wa nchi hiyo, iliyoandikwa na balozi wake wa Umoja wa Mataifa na kuelekezwa kwa Baraza la Usalama.

Barua hiyo inaeleza kuwa huku wapiganani wa TPLF "wakiwa wamezuiwa kwa kiasi kikubwa", serikali za Asmara na Addis Ababa zimekubaliana katika kiasi kikubwa kuanza kuondolewa kwa vikosi vya Eritrea.

Soma pia: UN: Ubakaji unatumiwa kama silaha za vita Tigray

Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed aliwapeleka wanajeshi katika eneo la machafuko la Tigray mnamo Novemba kwa lengo la kuwapokonya silaha na kuwadhibiti viongozi wa chama cha kisiasa kilichokuwa kikitawala katika mkoa huo, Tigray People's Liberation Front (TPLF).

Bildergalerie Äthiopien | Flucht aus der Region Tigray
Hali ya kibinadamu Tigray ni ya kutia wasiwasiPicha: Baz Ratner/REUTERS

Kwa miezi kadhaa serikali za Ethiopia na Eritrea zilikanusha kuwa Waeritrea walihusika katika operesheni hiyo, wakitofautiana na simulizi za wakaazi, mashirika ya haki, wafanyakazi wa misaada, wanadiplomasia na hata maafisa kadhaa wa kiraia na kijeshi wa Ethiopia.

Abiy hatimaye akakiri uwepo wa wanajeshi wa Eritrea mwezi Machi wakati akiwahutubia wabunge, na akaapa muda mfupi baadae kuwa wangeondoka.

Alhamisi, Mkuu wa misaada wa Umoja wa Mataifa Mark Lowock aliliambia Baraza la Usalama kuwa licha ya ahadi ya awali ya Abiy, haklujawa na ushahidi wa kujiondoa wanajeshi wa Eritrea katika jimbo hilo

Pia alisema wahudumu wa misaada wanaendelea kuripoti matukio mapya ya ukatili ambayo wanasema yanafanywa na Vikosi Vya Ulinzi vya Eritrea.

Soma pia:Marekani yahimiza kupunguzwa mzozo kati ya Sudan na Ethiopia

Waziri wa habari wa Eritrea Yemane Gebremeskel amesema leo kwenye Twitter kuwa Asmara imemuita mratibu mkaazi wa Umoja wa Mataifa nchini Eritrea na mkuu wa ofisi ya uratibu wa misaada ya Umoja wa Mataifa kulalamikia mazoea mabaya na ripoti za udanganyifu kwa misingi ya mitandao isiyopendeza na ushirikiano na TPLF.

Wakaazi wa Tigray mara kwa mara wanawatuhumu Waeritrea kwa ubakaji wa halaiki na mauaji ya kikatili yakiwemo katika miji ya Axum na Dengolat. Eritrea na Ethiopia zinadai mgogoro huo ulitokana na mashambulizi ya TPLF kwenye vituo vya jeshi la shirikisho mwanzoni mwa Novemva na kuielezea operesheni yao kuwa ya kurejesha sheria na utaratibu.

"Utoaji wa msaada wa kiutu katika mkoa wa Tigray unaendelea vizuri na mpaka sasa, hakuna aliyekufa kutokana na njaa,” Amesema Mitiku Kassa, mkuu wa tume ya kitaifa ya Mikasa nchini Ethiopia.

Mapema leo, Abadi Girmay, mkuu wa kilimo wa serikali ya mpito ya Tigray iliyoteuliwa na Abiy, ameonya kuhusu mgogoro wa njaa kama shughuli za kilimo hazitoanza tena.

AFP