1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Abe akutana na kiongozi mkuu wa Iran Khamenei

Bruce Amani
13 Juni 2019

Waziri Mkuu wa Japan Shinzo Abe amekutana na kiongozi mkuu wa Iran Ayatollah Ali Khamenei, akilenga kutuliza mivutano kati ya Iran na Marekani

https://p.dw.com/p/3KJIb
Der iranische Präsident Hassan Rouhani (R) trifft den japanischen Premierminister Shinzo Abe
Picha: ISNA

Abe na Khamenei wamekutana leo asubuhi, ikiwa ni katika siku ya pili na ya mwisho ya ziara ya kihistoria ya waziri mkuu huyo mjini Tehran. Iran imekuwa katika mzozo mkubwa na Marekani tangu Rais wa Marekani Donald Trump alipoiondoa nchi yake mnamo Mei mwaka jana katika mkataba wa kihistoria wa nyuklia uliofikiwa mwaka wa 2015. Marekani kisha ikaweka vikwazo vipya na vikali ambavyo vimeilazimu Japan kusitisha ununuzi wake wa mafuta ya Iran – na pia ikapeleka manowari za kijeshi katika eneo la Ghuba.

Mzozo huo wa Ghuba imeifanya Saudi Arabia leo kuionya Iran kuhusu kutokea madhara makubwa, baada ya waasi wa Houthi nchini Yemen wanaoungwa mkono na Iran kuwajeruhi watu 26 katika shambulizi la kombora kwenye uwanja wa ndege wa Saudia.

Der iranische Präsident Hassan Rouhani (R) trifft den japanischen Premierminister Shinzo Abe
Abe na Rouhani walizungumzia mzozo wa Mashariki ya KatiPicha: Getty Images

Japan ni mshirika muhimu wa Marekani na tangu jadi imekuwa na mahusiano mazuri na Iran. Abe aliwaambia wanahabari jana baada ya kukutana na Rais Hassan Rouhani kuwa ni muhimu kwa Iran kuwa na jukumu muhimu la kujenga Amani na utulivu katika Mashariki ya Kati

"Napenda kutoa heshima zangu za dhati kutokana na ukweli kwamba Kiongozi Mkuu Ayatollah Khamenei amesisitiza kuhusu tamko la kidini fatwa ambalo linasema silaha za nyuklia na silaha nyingine za maangamizi ni kinyume na Uislamu".

Akihutubia kikao hicho cha habari, Rouhani alisema anatarajia mabadiliko mazuri kufanyika katika Mashariki ya Kati na ulimwengu kama Marekani itasitisha shinikizo la kiuchumi dhidi ya Iran kupitia vikwazo. "Hatutaanzisha mgogoro katika kanda hii, hata dhidi ya Marekani, lakini kama vita vitaanzishwa dhidi yetu, basi nasi tutajibu vikali". Alisema Rouhani

Abe alianza ziara yake jana nchini Iran ikiwa na lengo la kutuliza mvutano kati ya Iran na Marekani. Japan iliacha kununua mafuta ghafi ya Iran mwezi Mei ili kuheshimu vikwazo vya Marekani dhidi ya Jamuhuri hiyo ya Kiislamu.

Taifa hilo lenye nguvu barani Asia lina nia ya kuifanya kuwa tulivu kanda ya Mashariki ya Kati ili kuhakikisha kuwa kuna biashara nafuu ya bidhaa za mafuta na gesi kuendesha uchumi wake. Rouhani alisema Japan imeonyesha nia ya kutaka kuendelea na ununuzi wa mafuta kutoka Iran