1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waziri wa pili Ujerumani ajiweka karantini

24 Septemba 2020

Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani, Heiko Maas amejiweka karantini kutokana na kitisho cha virusi vya corona. Haya yanajiri wakati serikali imetoa wito kwa umma kutumia app yakugundua mtu aliyeambukizwa virusi hivyo

https://p.dw.com/p/3ivck
Coronavirus I Außenminister Heiko Maas
Picha: Thanassis Stavrakis/AP/dpa/picture-alliance

Kwa mujimu wa ofisi yake, Maas alianza kujiweka karantini baada ya kufahamika kwamba mmoja wa walinzi wake aliambukizwa virusi vya corona, ila kipimo cha kwanza alichofanyiwa waziri huyo mwenye miaka 54 kimeonyesha hana virusi hivyo. Soma pia: Ulaya inaweza kuepuka hatua za kuzuia COVID-19 kwa mara ya pili?

Haijabainika bado ni vipi hatua hiyo itakavyoathiri kazi za mwanadiplomasia huyo wa ngazi za juu wa Ujerumani. Hapo jana alifanya kazi na akashiriki mikutano kadhaa iliyofanyika kwa njia ya video.

Bundeswirtschaftsminister Peter Altmeier
Waziri wa uchumi Ujerumani Altmeier ajiweka karantiniPicha: Getty Images/AFP/A. Schmidt

Amefutilia mbali ziara zake kuelekea Amman, Jordan, ambapo alikuwa akutane na mawaziri wa mambo ya nje wa Ufaransa na Jordan.

Wakati huo huo, Waziri wa Biashara wa Ujerumani, Peter Altmaier kupitia ujumbe aliouandika kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter, amesema kwamba amejiweka karantini. Hii ni baada ya kufahamu kwamba mmoja wa wafanyakazi wa waziri mmoja katika mkutano wa mawaziri wa biashara mjini Berlin amegunduliwa kuwa na virusi vya corona. Soma pia: Polisi Berlin yavunja maandamano ya kupinga vizuizi vya corona

Altmaier alifanyiwa vipimo Ijumaa ila hakupatikana na virusi hivyo na anasema anaendelea vyema. Hapo jana ilikuwa siku ya 100 tangu kuzinduliwa kwa app ya kugundua walioathirika na virusi vya corona nchini Ujerumani na Waziri wa Afya, Jens Spahn ametoa wito kwa kila mmoja kuitumia app hiyo. App hiyo inamfahamisha mtumiaji kama amekutana na mtu mwenye virusi hivyo.

Kwengineko Ulaya, Waziri Mkuu wa Ubelgiji, Sophie Wilmes amesema haitokuwa lazima kuvaa barakoa nchini humo kuanzia Oktoba mosi. Ilikuwa ni lazima kuvaa barakoa katika miji kadhaa ya Ubelgiji ukiwemo mji mkuu, Brussels ila Wilmes sasa anasema hakuna haja ya kuwalazimisha watu kuvaa barakoa kila mahali.

Deutschland | Corona Warn-App | Symbolbild
App ya kuonya kuhusu maambukizi ya coronaPicha: picture-alliance/dpa/M. Kappeler

Hayo yakiarifiwa Rais wa Iraq, Barhem Saleh ameuambia Umoja wa Mataifa kwamba nchi yake inahitaji usaidizi wa kimataifa kuzuia kuenea kwa virusi vya corona. Saleh anasema miundombinu duni nchini mwake pamoja na kushuka kwa bei za mafuta ni mambo yaliyoiweka nchi hiyo pabaya. Soma pia: Majaribio ya chanjo ya corona kuanza tena

Naye Waziri Mkuu wa Canada, Justin Trudeau amesema wimbi la pili la maambukizi nchini mwake limeanza tayari na anaonya kuwa hali itakuwa mbaya zaidi katika msimu wa mapukutiko kuliko ilivyokuwa katika kipindi cha machipuko.

Huko Brazil nako, utafiti uliochapishwa na tovuti ya MedRxiv umeonyesha kuwa huenda ikawa miili ya wakaazi wa mji wa Manaus ulioathirika vibaya mno na virusi hivyo imejiwekea kinga hivyo basi virusi hivyo haviwezi kusambaa tena miongoni mwao kama ilivyokuwa awali. Utafiti huo unasema asilimia 66 ya wakaazi hao wana kinga ya virusi vya corona.

afp, ap, reuters, dpa