1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waziri Mkuu wa Sudan afanya mabadiliko ya mawaziri

10 Julai 2020

Waziri Mkuu wa Sudan Abdullah Hamduk amefanya mabadiliko katika baraza la mawaziri baada ya miito ya mageuzi ya kisiasa kutolewa.

https://p.dw.com/p/3f5rw
USA Regierungschef der Übergangsregierung in Sudan Abdullah Hamduk
Picha: AFP/J. Watson

Kwa mujibu wa taarifa ya serikali, Waziri Mkuu huyo amekubali kujiuzulu kwa mawaziri sita wakiwemo waziri wa mambo ya nje, fedha, kilimo, nishati na uchukuzi.

Baada ya kujiuzulu kwa mawaziri hao, wizara hizo sasa zitasimamiwa na manaibu wake hadi uteuzi mpya utakapofanyika, taarifa hiyo imeongeza.

Mabadiliko hayo yanafanyika baada ya maelfu ya waandamanaji mwishoni mwa mwezi Juni kushinikiza kufanyika mageuzi ya haraka ya kisiasa ikiwemo kubuniwa kwa bunge, mageuzi katika vikosi vya usalama na uwepo wa idara huru ya mahakama.

Nchi hiyo imeshuhudiwa wimbi kubwa la mabadiliko ya kisiasa baada ya kung'olewa madarakani kwa Rais Omar al- Bashir Aprili mwaka 2019.