1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wavulana milioni 115 duniani kote waliingia ndoa za utotoni

Sylvia Mwehozi
7 Juni 2019

Shirika la Umoja wa Mataifa linalojihusisha na masuala ya watoto UNICEF, limesema katika ripoti yake mpya kwamba kiasi ya wavulana milioni 115 duniani kote waliingia katika ndoa za mapema.

https://p.dw.com/p/3K2bd
Kinderehe in Indien
Picha: picture alliance/AP Photo/P. Hatvalne

Ndoa za utotoni ni tatizo linalowakumba wasichana kwa wavulana na kuathiri fursa ya wanandoa hao watoto kupata elimu sahihi na fursa za kazi. Wavulana milioni 115 duniani kote walio na umri wa kati ya miaka 20 na 24 walioa kabla ya kufikisha umri wa miaka 18 kwa mujibu wa ripoti ya UNICEF.  Mvulana mmoja kati ya watano kati ya idadi hiyo alikuwa chini ya miaka 15.

Utafiti huo wa kwanza kuangazia ndoa za mapema kwa upande wa wavulana, uliendeshwa katika jumla ya nchi 82 na ulibaini kuwa Jamhuri ya Afrika ya Kati inaongoza kwa ndoa za aina hiyo kwa asilimia 28 ikifuatiwa na Nicaragua asilimia 19 na Madagscar iko nafasi ya tatu na asilimia 13.

Kinderehe in Indien
Bwana harusi miaka 16 na bibi harusi mwenye miaka 11 baada ya kufunga ndoa IndiaPicha: picture alliance/AP Photo/P. Hatvalne

Kwenye taarifa yake, Mkurugenzi wa UNICEF Henrietta Fore alisisitiza juu ya athari za ndoa za mapema katika  ustawi wa wavulana, na kusema kwmaba kitendo hicho kinapora utoto wao. "Mabwana harusi wavulana wanalazimika kuchukua majukumu ya kiutu uzima ambayo wengi bado wanakuwa hawako tayari. Ndoa za mapema zinaleta majukumu ya mapema ya ubaba na kuongeza shinikizo la kuihudumia familia, na hivyo kupunguza fursa za elimu na kazi." Naye mkurugenzi wa chama cha waandishi wa habari Tanzania Tamwa, Soma zaidi...

Aidha UNICEF inadai kuwa wasichana wameendelea kuolewa katika umri mdogo ambapo binti mmoja kati ya watano katika umri wa kati ya miaka 20 na 24 aliolewa kabla ya kufikisha miaka 18 ukilinganisha na mvulana mmoja kati ya 30. Ripoti hiyo itaja jumla ya watoto milioni 756 duniani kote wavulana kwa wasiichana walioingia katika ndoa za umri mdogo.

Ripoti hiyo zaidi ilibaini kwamba watoto wanaoa au kuolewa mapema hushindwa kuendelea na shule na hivyo kukosa fursa za kiuchumi na pia kuwa katika hatari ya kunyanyaswa na kuishia kupata matatizo ya afya ya akili ukilinganisha na wale waliooa au kuolewa katika umri wa utu uzima.

Bildergalerie Kinderheirat in Südasien
Bangladesh ina tatizo kubwa la ndoa za utotoni. Pichani ni wanaharakati wanaopingaPicha: picture-alliance/Pacific Press/M. Asad

Kama wasichana wote wangemaliza masomo ya sekondari, hiyo inamaanisha kwamba ndoa milioni 50 za mapema zingeweza kuepukwa kufikia mwaka 2030, kwa mujibu wa ripoti ya shirika la kimatifa Save the Children ya mwezi oktoba. Umoja wa Mataifa umezitolea wito nchi zote duniani kukomesha ndoa za utotoni kufikia mwaka 2030 kama ilivyokubaliwa katika malengo ya dunia ya maendeleo ya mwaka 2015. Angalau kila nchi inakabiliwa na tatizo la ndoa za utotoni lakini watoto wengi bado wanaolewa kwa mujibu wa sheria katika nchi kama vile Marekani ikiwa wazazi watatoa baraka zote au kupitia sherehe za kidini kwa mujibu wa kituo cha kutathmini sera za dunia.

Thomson Reuters Foundation