1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wapinzani wa waziri Imran Khan kuunda serikali ya muungano

Sudi Mnette
21 Februari 2024

Wapinzani wa kisiasa wa waziri mkuu wa zamani wa Pakistan aliyegerezani, Imran Khan wametangaza makubaliano ya mgawanyo wa madaraka kwa kulitaja jina la Shehbaz Sharif kuwa mgombea wao wa pamoja wa nafasi ya waziri mkuu.

https://p.dw.com/p/4cftp
Pakistan, Lahore | Shehbaz Sharif mkutano na waandishi wa habari
Waziri Mkuu wa zamani wa Pakistan Shehbaz Sharif akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari kuhusu uchaguzi wa bunge, huko Lahore, Pakistan, Jumanne, Februari 13, 2024.Picha: K.M. Chaudary/AP/picture alliance

Tangazo hilo lililosubiriwa kwa hamu limefuatia siku kadhaa za mazungumzo miongoni mwa uongozi wa vyama vya Pakistan Muslim League - PML, Pakistan Peoples - PPP, na vyama vingine ambavyo havikushinda viti vya kutosha katika uchaguzi wa Februari 8.

Wagombea wa upande wa Khan walishinda kwa wingi wa viti katika uchaguzi wa ubunge ingawa pia ushindi huo haukuwapa uwezo wa kutosha kuunda serikali.

Bunge kuamua kuhusu Shehbaz Sharif kuwa waziri mkuu mpya

Pakistan Karachi | Maandamano ya kupinga madai ya kudanganywa kwa uchaguzi baada ya uchaguzi wa bunge
Maandamano dhidi ya madai ya udanganyifu wa uchaguzi baada ya uchaguzi wa bunge Februari 17, 2024Picha: Rizwan Tabassum/AFP/Getty Images

Bunge litaamua iwapo litamchagua Shehbaz Sharif wa chama cha PML kuwa waziri mkuu mpya wakati kikao cha ufunguzi cha bunge kitakapoandaliwa baadae mwezi huu. Sharif, kaka ya waziri mkuu wa zamani Nawaz Sharif, naye pia ni waziri mkuu wa zamani, aliyechukua nafasi ya Khan alipoondolewa kupitia kura ya kutokuwa na imani naye bungeni mwaka wa 2022.

Tangu wakati huo, Khan ametiwa hatiani kwamakosa kadhaa katika kile wafuasi wake wanachokiita kesi zilizopandikizwa kisiasa kumfanya asiwe nje ya ofisi. Katika mkutano wao uliofanyika hadi usiku wa manane wapinzani wa Khan walisema kwamba walikuwa wamepata wingi wa kura zinazohitajika ili kuunda a serikali ya muungano.

Ombi la Kujiuzulu kwa Mkuu wa Tume ya Uchaguzi ya Pakistan, Sikandar Sultan Raja

Aidha, rais wa zamani Asif Ali Zardari wa PPP atakuwa mgombea wa pamoja wa ofisi ya rais wakati bunge jipya na mabunge yote manne ya mikoa yatakapomchagua mrithi wa Rais anayeondoka Arif Ali wiki chache zijazo. Mapema Jumanne, chama cha Khan cha Pakistan Tehreek-e-Insaf kiliomba kujiuzulu kwa mkuu wa Tume ya Uchaguzi ya Pakistan, Sikandar Sultan Raja, kwa madai ya kushindwa kuendesha uchaguzi huo kwa uhuru na namna ya haki.

Mapema Jumanne, chama cha Khan cha Pakistan Tehreek-e-Insaf kiliomba kujiuzulu kwa mkuu wa Tume ya Uchaguzi ya Pakistan, Sikandar Sultan Raja, kwa madai ya kushindwa kuendesha uchaguzi huo kwa uhuru na namna ya haki. Ingawa wagombea wa Khan walishinda viti 93 kati ya 265 vya Bunge la Kitaifa, hatua ambayo imeifanya kishindwa kuunda serikali.

Soma zaidi:Matokeo ya awali yawapa ushindi wafuasi wa Imran Khan

Khan anatumikia vifungo kadhaa baada ya kuhukumiwa jumla ya miaka 31 jela kwa makosa ya rushwa, kufichua siri za serikali na ukiukwaji wa sheria ya ndoa mwishoni mwa Januari na mapema Februari.