Wahariri wanatumai Tymoshenko atapata matibabu nchini Ujerumani
10 Mei 2012Juu ya mogogoro wa Ugiriki gazeti la "Cellesche Zeitung" linauliza, jee Ugiriki bado inaweza kuokolewa? Na anasema kwa sasa mambo hayaonekani kuwa hivyo. Lakini anatahadharisha kwamba ikiwa Ugiriki itafilisika, watakaothirika sana hawatakuwa Wagiriki tu, bali sarafu ya Euro pia itaathirika.
Sarafu hiyo ilipaswa kuthaminiwa duniani kote. Lakini lengo hilo bado lipo mbali sana ,na hasa kwa sababu katika nchi nyingine za Ulaya watetezi wa sera ya kubana matumizi wamesimama kidete kuitetea sera hiyo.
Naye mhariri wa gazeti la "Emder Zeitung " anasema kinachoonekana nchini Ugiriki sasa ni tamthilia ya tanzia. Wagiriki wamejitumbukiza katika maafa, kiasi kwamba inashindikana kuwasaidia. Mhariri huyo anaeleza kuwa Wagiriki wamejiingiza katika mtego kiasi kwamba juhudi zote za kuwaokoa zinaonekana kuwa ni kazi bure. Na jambo la kusikitisha ni kwamba Wagiriki wenyewe wanafanya iwe vigumu hata kwa wale wenye nia njema ya kusaidia.
Gazeti la "Rhein-Neckar-Zeitung" linasema kauli ya kiongozi wa chama cha mrengo wa shoto nchini Ugiriki juu ya nchi hiyo kutoyalipa madeni yake ,ni ya kutia wasiwasi. Ndiyo sababu kwamba Umoja wa Ulaya unapaswa kuimarisha shinikizo. Gazeti hilo linahoji kuwa sasa pana mawanda finyu baina ya kusambaratika kwa sarafu ya Euro na juhudi za uokozi. Na hasa kwa sababu hakuna anaeweza kuwazuia Wagiriki kuiteketeza nchi yao kiuchumi na athari zake zote kwa nchi zote za Ulaya.
Gazeti la "Badische Zeitung"linaeleza kuwa dhamira ya kuzipa nchi za kusini mwa Ulaya matumaini ipo. Lakini ukweli ni kwamba uwezekano siyo mkubwa. Mhariri wa gazeti hilo anasema, agizo lililotolewa kwa Benki ya Ulaya ya vitega uchumi, kuekeza Euro Bilioni 60 linaonyesha hali ya kutamauka, hata ikiwa fedha hizo zitatolewa na kutumiwa kwa busara. Lakini ili kurejesha ustawi,hatua nyingi zaidi zinalazimu kuchukuliwa.
Mhariri wa gazeti la "Stuttgarter Nachrichten"anatoa maoni juu ya kiongozi wa upinzani nchini Ukraine, Yulia Tymomshenko ambae hapo awali aligoma kula ikiwa ni ishara ya kupinga udhalimu anaotendewa jela.Mhariri wa gazeti hilo anatilia maanani kwamba sasa mwanasiasa huyo aliewahi kuwa Waziri Mkuu wa Ukraine, ameuacha mgogo wake. Ameanza kula tena na ametembelewa na daktari kutoka Ujerumani. Viongozi wa Ukraine pia wameashiria matumaini ya mwanasiasa huyo kupatiwa matibabu zaidi nchini Ujerumani.Umoja wa Ulaya umepata ushindi katika raundi ya kwanza. Hata hivyo yapasa kuwa macho, kwani hatua ya Rais Yanukovitch ya kulegeza kamba kidogo haina maana kwamba sasa Rais huyo amekuwa mpenda demokrasia.
Mwandishi:Mtullya abdu.Deutsche zeitungen.
Mhariri: Miraji Othman