Ufaransa kuandaa mkutano wa dharura wa DRC Oktoba
24 Septemba 2025
Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo Felix Tshisekedi ameziomba nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa kutambua kile alichokiita "mauaji ya kimya kimya" katika nchi yake. Kauli hiyo inafuatia tangazo la Ufaransa la kuwa mwenyeji wa mkutano wa dharura kuhusu mzozo wa Kongo mwezi ujao.
Akizungumza katika mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa,Tshisekedi amesema vita nchini mwake vimewaathiri watu wa Kongo kwa zaidi ya miaka thelathini na ametoa wito kwa tume huru ya kimataifa ya uchunguzi kusaidia kutafuta suluhisho la kiini cha mzozo wa mashariki mwa nchi hiyo.
Kwa upande wake, Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron amesema mkutano huo wa dharura utakaofanyika Paris, utawaleta pamoja wote ambao wanaweza kushughulikia dharura ya kiutu na kuchangia katika juhudi na mipango ya amani ambayo tayari inaendelea.