Tanzania yatafuta uponyaji baada ya vurugu za Uchaguzi Mkuu
11 Novemba 2025
Ni dhahiri kuwa macho ya watoto yaliona zaidi ya kile ambacho macho yao yanavyoweza kustahimili. Walishuhudia ndugu wakijeruhiwa, walisikia milio ya risasi, mabomu ya machozi na keleleza waandamanaji. Kwa umri wao hizi ni kumbukumbu zinazoweza kubaki kwa muda mrefu.
Vurugu za Oktoba 29 hazikuacha makovu kwa wanaume na wanawake tu bali hata kwa Watoto.Ambao wamekuwa na maswali lukuki juu ya nini kilichosababisha, na nini kitafuata.
"Watoto wana hofu kubwa"
Joyna Mapungu, ni mzazi na mkazi wa Kimara, Dar es Salaam "Kwa kweli watoto walikuwa na hofu kubwa hata ukitaka kutoka watoto wanapiga kelele. Halafu kuna kitu kingine mimi kilinishangaza siku moja mtoto wangu alitoka nje na hakuona mtu yoyote akarudi ndani mbio akiwa na hofu akauliza mama watu wameenda wapi,?"
Wataalamu wa afya ya akili wanasema matukio kama haya yanaweza kusababisha kiwewe cha kisaikolojia kwa watoto.Wengine wanaanza kujitenga na wenzao, wengine hukataa kwenda shule au kushindwa kuzungumza kabisa, kama mwanasaikolojia Saldine Kimangale anavyosema. "Watoto huwa wana'react' tofauti kwa sababu wao hawana njia sahihi ya kueleza hisia zao.. kwa hiyo mara nyingi unaweza kuona wao wanakuwa na mabadiliko ya tabia ambayo hayakutarajiwa. Kwa mfano unaweza kuona mtoto labda ameanzisha tabia ya kulialia..."
Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025 uligubikwa na vurugu za maandamano ya vijana waliokuwa wakidai haki. Vurugu hizo ziliviinua vyombo vya ulinzi na usalama ambao walichukua hatua na kusababisha kuwepo kwa milio ya risasi, mabomu na mauaji ya watu.
Watahiniwa wapewa fursa maalumu ya kuikabili hofu na wasiwasi
Haya yote yanajiri wakati ambapo wanafunzi wa kidato cha pili wanatarajia kuanza mitihani yao ya taifa, Jumatatu Novemba 10 badala ya Novemba 3, na Kidato cha nne wakitarajiwa kuanza mitihani yao Novemba 24 badala ya Novemba 17.
Ili kuweka hali hasa kwa watahiniwa, Mwalimu Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Mugabe jijini Dar es Salaam amesema imewalazimu kuzungumza na watahiniwa ili kuwatoa kwenye athari za kisaikolojia kabla ya mitihani. Mwalimu Mathewe Mchome alipozungumza na DW alisema "Tumetengeneza timu ya walimu ambao sisi tunaamini kwa uelewa wao wanaweza kutambua watoto wanaoonekana kuwa na msongo wa mawazo kidogo." Akaongeza kuwa wanaangalia namna ya kuingiza masuala ya amani kwenye baadhi ya masomo.
Mashirika ya kiraia yanatoa wito kwa serikali na wadau wa maendeleo kuweka mipango ya ushauri nasaha, hasa kwa watoto waliokuwa mashuhuda wa vurugu hizo. Kwao, si tu matukio ya kisiasa—ni ndoto mbaya zinazoweza kuendelea hata baada ya nchi kurudi katika utulivu.
Wataalamu wanasema, kuponya makovu ya risasi ni rahisi kuliko kuponya makovu ya nafsi. Watoto hawa wanahitaji zaidi ya ukimya na muda, wanahitaji kusikilizwa, kuhurumiwa na kusaidiwa kurejea katika hali yao ya kawaida.