1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Sudan: Al-Bashir huenda amejiuzulu, jeshi kutoa taarifa

Sekione Kitojo
11 Aprili 2019

Taarifa nchini Sudan zinasema rais Omar al-Bashir amelazimishwa na jeshi kujiuzulu,na jeshi la nchi hiyo limesema lingetoa taarifa muhimu hivi karibuni. Haya yanafuatia miezi kadhaa ya maandamano dhidi ya Bashir.

https://p.dw.com/p/3Gbfq
Sudan Proteste gegen Präsident Omar Al-Bashir in Khartoum
Waandamanaji wakionesha alama ya ushindi baada ya kupata taarifa kuwa jeshi litatoa taarifa muhimu hivi karibuni nchini SudanPicha: Reuters

Maelfu  ya  wakaazi  wa  mjini  Khartoum waliimba, "utawala umeanguka"  wakati  wakimiminika  katika  eneo  kuzunguka makao makuu  ya  jeshi  ambako  waandamanaji  wamekuwa wakikaa  hapo kwa  muda  wa  siku  sita sasa.

Sudan Proteste gegen Präsident Omar Al-Bashir in Khartoum
Waandamanaji mjini Khartoum wakishangiria baada ya kusikia kwamba jeshi la nchi hiyo litatoa taarifa muhimu hivi karibuni.Picha: Reuters

"Jeshi  la  Sudan  litatoa  taarifa  muhimu  hivi  karibuni. Subirini, mtangazaji  wa  televisheni  ya  taifa  alisema, bila  ya  kutoa maelezo  zaidi. Mtu ambaye haikuelezwa  ni  nani  alisema.

"Watazamaji  wa  televisheni  ya Sudan , katika  muda  mfupi ujao jeshi  litatoa  taarifa  muhimu"

Muziki  wa  kijeshi  umechukua  nafasi  ya  matangazo  ya  kawaida katika  televisheni. 'Hatutaondoka  hapa  hadi tutakapofahamu  ni kitu  gani jeshi  litatuambia. Lakini  tunafahamu  kwamba  Bashir lazima  aondoke. Tunasubiri taarifa  muhimu,' mmoja  kati  ya waandamanaji  aliliambia  shirika  la  habari  la  AFP  kutoka  katika eneo ambalo  waandamanaji  wamekita  kambi. Tumechoshwa na utawala  huu , miaka  30 ya ukandamizaji, rushwa , ukiukaji  wa  haki za  binadamu, imetosha, amengeza mtu huo.

Sudan Proteste in Karthoum
Waandamanaji mjini Khartoum wakishangiria na wakiwa wamewashirikisha hadi watoto ikiwa ni ishara ya maandamano ya amani ya kumshinikiza raisBashir kuondoka madarakaniPicha: picture alliance/AA

Maandamano, ambayo  yalizuka  Desemba, yamekuwa  changamoto kubwa  hadi  hivi  sasa  katika  utawala  wa  miongo  mitatu  wa Bashir wa  mkono  wa  chuma.

Kundi  la  wandamanaji limekuwa  likiishi kwa  siku  tano  nje  ya makao  makuu  ya  jeshi, eneo  ambalo  pia  ni makao  rasmi  ya rais  Bashir  na  wizara  ya  ulinzi.

Kumekuwa  na  hali  ya  sherehe  katika  eneo  hilo, ambalo waandamanaji  wanaimba  na  kucheza  nyimbo za  kimapinduzi.

Magari  kadhaa  ya  kijeshi  yakiwa  na  wanajeshi  yaliingia  katika eneo  hilo  la  jeshi mapema  leo , kwa  mujibu  wa  watu walioshuhudia.

Sudan Omar Al-Bashir
Rais Omar al-Bashir ambaye anashinikizwa na waandamanaji kujiuzulu baada ya utawala wake wa zaidi ya miaka 30 nchini SudanPicha: Reuters/M. N. Abdallah

Wamesema  magari  mengi  ya  jeshi yakiwa  na  wanajeshi yamewekwa  katikati  ya  Khartoum  mapema  leo.

kundi  linaloongoza  maandamano  ya  nchi  nzima  limewataka wakaazi  wa  mji  mkuu Khartoum  na  kwingineko  kujazana  nje  ya makao  makuu  ya  jeshi. Mtandao  wa  televisheni  za  mataifa  ya Kiarabu  ulitangaza ripoti  ambazo  hazijathibitishwa  kwamba Omar al-Bashir  amejiuzulu  na  kwamba  maafisa  wa  ngazi  ya  juu  wa chama  tawala  pia  wanakamatwa.

Mahali  alipo  kiongozi  huyo dikteta , ambaye  ametengwa  na mataifa  mengi  na  pia  anatakiwa   na  mahakama  ya  kimataifa  ya uhalifu  kwa mauaji  katika  jimbo  la  Darfur, bado  hakujulikani.