1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Serikali za kaunti Kenya kusitisha utoaji wa huduma mikoani

Sylvia Mwehozi
17 Septemba 2020

Wakenya huenda wakakabiliana na hali ngumu baada ya serikali za kaunti kusitisha utoaji wa huduma mikoani kwasababu ya uhaba wa fedha na wafanyakazi wake kuchukua likizo ya wiki mbili.

https://p.dw.com/p/3id2N
Kenia | Nairobi | Smog | Luftverschmutzung
Picha: picture-alliance/AP Photo/S. A. Azim

Haya yanajiri wakati ambapo mzozo wa ugavi wa fedha kwa serikali za kaunti kukosa suluhu hata baada ya baraza la Senate kufanya vikao 10 bila mafanikio.Tatizo liliibuka baada ya maseneta kushindwa kuafikiana kuhusu mfumo wa ugavi ama kwa kuzingatia idadi ya wakaazi au ukubwa wa kaunti.

Huduma za umma za mikoani zimesitishwa kwasababu ya uhaba wa fedha unaozikumba serikali za kaunti. Kwenye taarifa yake ya saa chache zilizopita,mwenyekiti wa baraza la magavana, Wycliffe Oparanya, alifafanua kuwa kilichochangia hatua hiyo ni uhaba wa nyenzo na vitendea kazi baada ya maseneta kushindwa kufikia mwafaka wa ugavi wa fedha za kaunti.

Gavana Oparanya ameonya kuwa serikali za kaunti zinakabiliana na hali ngumu kutokana na kukosa fedha na wanashindwa kulipa mishahara.Gavana wa Makueni Kivutha Kibwana na mwenzake wa West Pokot John Lonyang'apuo wanamuunga mkono mwenyekiti wa baraza lao kwa kuchukua hatua ya kusitisha huduma za kaunti.

Kwa sasa vituo vya afya vinavyosimamiwa na kaunti havitatoa huduma kwa wagonjwa wa kulazwa. Watakaohudumiwa ni wachache wanaohitaji usaidizi na kurejea nyumbani.Kadhalika wafanyakazi wa kaunti wa huduma zisokuwa za msingi wameagizwa kwenda likizo kwa wiki mbili.Gavana wa kaunti ya Machakos Alfred Mutua anasisitiza kuwa hii ndiyo njia ya pekee.

Afrika Airlines | Kenia - Kenya Airways Boeing 787
Ndege ya shirika la ndege la KenyaPicha: picture-alliance/M. Mainka

Yote hayo yakiendelea,kulizuka kivumbi kwenye kikao cha baraza la Senate saa chache zilizopita.Maseneta walinyoosheana vidole vya lawama na cheche za maneno. Kiranja ya chama tawala kwenye baraza la Senate Irungu Kangata aliwakosoa magavana kwa kuchukua hatua ya kusitisha huduma kwenye kaunti. Seneta Kangata aliwashutumu magavana kwa kutowasilishwa suala hilo kwenye kikao na rais mwanzoni mwa wiki hii.

Itakumbukwa kuwa siku ya Jumanne Rais Uhuru Kenyattaalifanya kikao maalum cha baraza la mawaziri na magavana waliwakilishwa na mwenyekiti wa baraza lao Wycliff Oparanya.Hicho kilikuwa kikao cha kumi cha kusaka suluhu ya mzozo huo bila mafanikio.

Kwenye kikao hicho Rais Uhuru Kenyatta aliahidi kuzitengea kaunti shilingi bilioni 50 za ziada katika mwaka wa fedha ujao ili kuzisaidia serikali ambazo zinapunguziwa hela kuhimili dhoruba zozote.Ifahamike kuwa serikali za kaunti zinayo ridhaa ya kupokea 50% ya fedha zilizotengewa kwenye bajeti ya mwaka huu wa fedha.Hata hivyo waziri wa fedha wa Kenya Ukur Yattani bado hajaweza kuruhuse hela hizo kuhamishwa kwa serikali za kaunti.

Wiki iliyopita mratibu wa bajeti Margaret Nyakango alibainisha kuwa afisi yake haina uwezo wa kuruhusu fedha hizo kuhamishwa kwa serikali za kaunti kwani bado ziko mikononi mwa hazina maalum ya kitaifa.TM,DW Nairobi.

Thelma Mwdzaya