1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

River Plate mabingwa wa Copa Libertadores

Sekione Kitojo
10 Desemba 2018

River Plate  ya  Argentina  yaibuka  nayo  kidedea  katika mpambano  wa  watani  wa  jadi  na  kuibuka  mabingwa  wa  Copa Libertadores dhidi  ya  Boca  Junior.

https://p.dw.com/p/39otm
Copa Libertadores 2018  River Plate Sieger Jubel
Mabingwa wa kombe la America kusini la Copa Libertadores River PlatePicha: Reuters/J. Medina

Copa Lebertadores kombe  la  mabingwa  wa   mataifa  ya  America ya  kusini  sawa  na  Champions  League  barani  Ulaya  ama Champions League  barani  Afrika  mara  hii  limekwenda  kwa  River Plate  ya  Argentina , baada  ya  mpambano  mkali  na  wa  kukata na  shoka  wa  mkondo  wa  pili   jana  Jumapili  baina  ya  mahasimu wakubwa  wa  mji  mmoja  Buenos Aires , Boca  Juniors  na  River Plate  kukipiga  hapo  jana  katika  uwanja  wa  Santiago  Beunabeu mjini  Madrid.  Nyasi  ziliwaka  moto  jana usiku......

Champions-League-Finale Südamerika River Plate - Boca Juniors 1:1
Wachezaji wa River Plate wakishangiria bao baada ya kupata bao la kusawazisha dhidi ya Boca Juniors pia ya ArgentinaPicha: picture-alliance/dpa/C. de Luca

Mchezo  ulichezwa  mjini  Madrid  lakini  sherehe  na  majonzi yalibakia  nchini  Argentina.  River Plate  ilishinda  mashindano  ya Copa Libertadores kwa  kuwashinda  mahasimu  wao  wakubwa Boca  Juniors  katika  fainali  ambayo  ilidumu  kwa  mwezi  mzima na  kuhamishiwa  nchini Uhispania  kwa  mara  ya  kwanza  katika historia  kwasabbu  ya  ghasia  za  mashabiki  kabla  ya  mchezo  wa mkondo  wa  pili. 

Licha  ya  kuwa  uamuzi  huo  wa  shirikisho  la kandanda  la  Argentina  kuhamisha  mchezo  huo  uliwakasirisha Wargentina  wengi , lakini  kila  kundi  la  mashabiki  liliiangalia fainali  hiyo  kwa  hamasa, nguvu  na hisia  na  wendawazimu  kama ambavyo  mchezo  huo  ungefanyika  katika  ardhi  ya  America kusini. mashabiki  wa  River  Plate  walimiminika   katika  eneo  la wazi  la  Obelisk  katikati ya  jiji  la  Buenos Aires  jana  usiku kuishangiria  timu  yao  ikitawazwa  mabingwa  wa  Copa Libertadores.

"Wametuondoa  kutoka  uwanja  wetu, wametuondoa  kutoka  nchini mwetu, wameleta  vurugu  kubwa, na  tumeshinda pamoja  na  hayo. Imetosha  Boca. Hamna  cha  kusema. Tumewashinda kila  mahali."

Ushindi ni raha sana

Ilikuwa  ni  furaha  kila  kona  ya  jiji  la  Buenos Aires  ambalo lilitekwa  na  mashibiki  wa  River  Plate

Copa Libertadores Finale Südamerika River Plate - Boca Juniors 3:1 Martinez
Mshambuliaji Gonzalo Martinez akishangiria baada ya kupachika bao la 3 kwa River PlatePicha: Reuters/J. Medina

Uwanja  huo  wa  mjini  Madrid  ambao pia  utakuwa  mwenyeji  wa fainali  ya  Champions  League  barani  Ulaya  mwezi  Juni , uliteuliwa  kwa  sehemu  fulani  kwasababu  ya  rekodi  yake  ya kuwa  mwenyeji  wa  matukio  makubwa  na  usalama, ambao  ni pamoja  na  polisi 2,500  kuwekwa , ili  kulinda  usalama  kabla  ya mtanange  huo  kuanza.

Mashabiki  walitenganishwa  katika  kanda kila  upande  wa  uwanja na  walifanyiwa  ukaguzi  mkali. Vilabu  vyote  vilipewa  tikiti 25,000, na  ni 5,000  tu zilizotengwa  kwa  mashabiki  wanaoishi Argentina.

Huyu  hapa  shabiki  wa  River Plate Sofia  akiwa  mjini  Buenos Aires  akizungumza  baada  ya  mpambano  huo.

"Ni furaha  kubwa  mno, ushindi umeniondolea  mzigo baada  ya kukosa  usingizi kwa  wiki  kadhaa, kupoteza  sauti, na  kukosa  siku kadhaa  za  kwenda  kazini  kwasababu  nilikwenda  katika  michezo miwili  ambayo  iliahirishwa lakini  furaha  niliyonayo  ni  kubwa,  na hakuna  kinachonipa  faraja  kubwa  kuliko  kuvaa  jezi  hii."

River Plate v Boca Juniors - Copa CONMEBOL Libertadores 2018
Wachezaji wa Boca Juniors wakishangiria bao la kuongoza dhidi ya River Plate, lakini halikusaidia kuleta ushindiPicha: Getty Images/Ch. Brunskill

Wakati  huo  huo baada  ya  kuiongoza  River Plate  katika  ubingwa wao  wa  pili  wa  Copa Libertadores  katika  misimu  minne, kocha Marcelo Gallardo  anaonekana  kuwa  ataelekea  katika  mataifa  ya Ulaya  lakini  wachezaji  wake  wana  matumaini  kwamba  uhusiano wake  na  vigogo  hivyo  vya  soka  vya  Argentina  utamfanya abakie  mjini  Buenos Aires  kwa  kipindi  kirefu  kidogo. Atakwenda Ulaya  ktika  wakati  fulani, lakini  kwa  sasa  yuko  nyumbani  na  ni vigumu kwake  kuondoka," nahodha  wa  River Plate Leonardo Ponzio  aliwaambia  waandishi  habari  baada  ya  ushindi  wa  River wa  mabao 3-1 dhidi  ya  mahasimu  wao  Boca  Juniors.

 

Mwandishi: Sekione  Kitojo / ape / dpae / rtre / afpe

Mhariri:  Yusuf Saumu