1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUrusi

Putin hana mpango wa kuivamia Poland na Latvia

Lilian Mtono
9 Februari 2024

Rais wa Urusi Vladimir Putin amesema hawana mpango wa kuivamia Poland, Latvia ama eneo jingine lolote na kwamba hawana nia yoyote ya kuvipanua vita vyake nchini Ukraine.

https://p.dw.com/p/4cCWr
Pichani ni Rais Vladimir Putin akizungumza wakati ywa mkutano wa mwaka na waandishi wa habari Disemba 14; 2023
Rais wa Urusi Vladimir Putin amesema hawana mpango wa kuivamia Poland, Latvia na mahali pengine kwa kuwa hawana maslahi na mataifa hayoPicha: Alexander Zemlianichenko/REUTERS

Rais Putin amesema hayo kwenye mahojiano na mtangazaji wa televisheni wa nchini Marekani Tucker Carlson yaliyorekodiwa siku ya Jumanne mjini Moscow.

Lakini amesisitiza kwamba watachukua hatua ikiwa Poland itaivamia Urusi na kuongeza kuwa hawana maslahi yoyote nchini humo wala Latvia na eneo jingine lolote na kwa maana hiyo hawaoni sababu ya kuwavamia.

Putin aidha ameyahakikishia mataifa ya magharibi kwamba kamwe Urusi haitashindwa katika vita vyake nchini Ukraine na kuitaka Jumuiya ya kujihami ya NATO kukubaliana na hatua ya Urusi ya kuyanyakua maeneo nchini humo. 

Putin amesema kwa msisitizo kwenye mahojiano na mtangazaji huyo mwenye misimamo ya mrengo wa kulia Carlson kwamba mataifa ya magharibi yanatakiwa kuelewa kwamba "hawawezi" kuiashinda Urusi nchini Ukraine.

Putin asema Urusi ni muhanga wa usaliti wa magharibi

Kwenye mahojiano hayo ya masaa mawili na Carlson aliyewahi kuwa mtangazaji wa kituo cha utangazaji cha Fox News, siku chache kabla ya kumbukumbu ya miaka miwili ya vita hivyo--- Putin amesema pia kwamba upo "uwezekano wa kufikiwa" makubaliano juu ya mwandishi wa Wall Street Evan Gershkovich anayezuiwa nchini Urusi.

Tucker Carlson
Mtangazaji wa nchini Marekani Tucker Carlson ni wa kwanza kutoka magharibi kuzungumza na Rais Vladimir Putin tangu mwaka 2019. Picha: Giorgio Viera/AFP/Getty Images

"Mambo kadhaa yanaweza kujadiliwa kupitia chaneli maalumu," amesema huku akisisitiza kwamba mwandishi huyo ni jasusi---- kitu ambacho Gershkovich na serikali ya Marekani wanakana kabisa.

Haya yalikuwa ni mahojiano ya kwanza ya ana kwa ana kati ya Putin na chombo cha habari cha magharibi tangu 2019.

Hata hivyo licha ya kumuuliza baadhi ya maswali magumu, lakini ilimpasa Carlson aliye karibu na Ikulu ya Whie House na Rais wa zamani wa Marekani Donald Trump kumsikiliza zaidi Putin ambaye alijaribu kumueleza kwa kina mtizamo wake kuhusu historia ya Urusi na kulielezea taifa hilo kama muhanga wa usaliti wa magharibi.

Soma pia: Biden and Scholz kujadiliana juu ya msaada mpya kwa Ukraine

Putin ameitetea kwa mara nyingine hatua yake ya kuivamia Ukraine na kusema mataifa ya magharibi sasa yanatambua kwamba Urusi haiwezi kuangushwa ülicha ya msaada wa Marekani, Ulaya na NATO.

Zelensky amfuta kazi mkuu wa majeshi

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky amemfukuza Mkuu wa Majeshi Valerii Zaluzhnyi, na kumteua Kanali Jenerali Oleksander Syrskyi, aliyekuwa kamanda wa vikosi vya ardhini.

Ukraine | Vita | Volodymyr Zelensky na Oleksandr Syrsky
Rais Volodymyr Zelensky akiwa na Mkuu mpya wa majeshi Oleksandr Syrsky. Zelensky amemfuta kazi aliyekuwa mkuu wa majeshi Valerii ZaluzhnyiPicha: Efrem Lukatsky/AP Photo/picture alliance

Tangu mwishoni mwa mwaka uliopita, vyombo vya habari vimekuwa vikiripoti juu ya kutoelewana kati ya Zelensky na Zaluzhnyi.

Siku ya Alhamisi, Zelensky aliandika kwenye mtandao wa kijamii kwamba amekutana na Zaluzhnyi na kumweleza juu ya hatua hiyo na kujadiliana juu ya mabadiliko yanayohitajika ndani ya jeshi lakini pia mtu anayefaa kuchukua nafasi hiyo.

Soma pia: Ukraine: Urusi ilitumia makombora iliyopewa na Korea Kaskazini.

Kwenye taarifa yake, Zaluzhnyi amesema alikuwa na mazungumzo ya kina na muhimu na Zelensky na kusema kwamba uamuzi huo ulifanyika kwa ajili ya kubadilisha mbinu na mikakati ya kivita

"Majukumu ya 2022 yanatofautiana na majukumu ya 2024. Kwa hivyo, kila mtu analazimika kubadilika na kuendana na uhalisia mpya pia, ili kushinda kwa pamoja pia," imesema taarifa yake.

Jenerali Zaluzhnyi, 50, aliteuliwa kuwa mkuu wa majeshi miezi michache tu kabla Urusi haijaivamia kikamilifu Ukraine Februari 2022.