1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Nigeria: Miaka 50 baada ya vita ya Biafra

Iddi Ssessanga
15 Januari 2020

Zaidi ya watu milioni moja waliuawa katika vita vya Biafra vilivyodumu kwa miezi 30. Athari za vita hivyo bado zingalipo hadi hii leo, ingawa kila kitu hakipo kama inavyoonekana, miaka 50 tangu kumalizika kwa vita hivyo.

https://p.dw.com/p/3WCcy
Unabhängigkeitsbestrebungen von Biafra
Picha: picture alliance/W. Dabkowski

Uchenna Chikwendu huzungumza kwa nadra kuhusu vita vya Biafra. Chikwendu mwenye umri wa miaka 67 anaishi Enugu, mji mkuu wa jimbo lenye jina sawa mashariki mwa Nigeria ambalo lilikuwa sehemu ya taifa lililojitangazia uhuru wake la Biafra. Wakati wa vita hiyo iliyoanza Julai 1967 na kumalizika Januari 15 1970, Chikwendu alikuwa msichana.

"Tulikuwa tunatembea mara kwa mara. Hakukuwa na magari. Yeyote aliekuwa nalo alikuwa akilificha jeshi lisije kulichukuwa. Haikuwa rahisi, tulikuwa tunatembea kwa miguu. Tulikwenda soko saa tisa alfajiri na kufika saa 11. Tulifanya manunuzi yetu haraka na tukiwa njiani kurudi nyumbani tulikuwa tunachukuw atahadhari kubwa ili tusionekane," anasema Chikwendu.

Nigeria Uchenna Chikwendu
Uchenna Chikwendu huzungumza kwa nadra kuhusu uzoefu wake wa vita ya Biafra.Picha: DW/K. Gänsler

Nigeria, taifa lenye makabila zaidi ya 250, lilipata uhuru wake kutoka kwa Uingereza mwaka 1960, wakati huo likiwa na jumla ya wakaazi milioni 45, ambapo eneo la kaskazini lilikuwa linakaliwa na jamii za Wahaussa na Fulani, kusini-magharibi waliweko Wayorubu na kusini-mashariki walikuwa wanaishi watu wa jamii ya Igbo. Haraka zikajitokeza nyufa, mapambano ya kuwania madaraka na upatikanaji wa rasilimali yakazuka.

Mapinduzi mawili ya kijeshi yalifuatana mwaka 1966: Kwanza, Majenerali wakiongozwa na Johnson Aguiyi-Ironsi, mu Igbo walimpindua waziri mkuu Abubakari Tafawa Balewa kutoka eneo la kaskazini. Miezi sita baadae, mapinduzi mengine yalifuatia, ambamo majenerali hasa kutoka kaskazini walishiriki. Baada ya machafuko makubwa ya kikabila, gavana wa kijeshi wa jimbo hilo la kusini-mashariki, Chukwuemeka Odumenwu Okukwu, alilitangaza jimbo hilo kuwa taifa huru Mei 30, 1967.

Nigeria yasalia kuwa  taifa lililogawika

Kilichofuatia vilikuwa vita, ambamo inakadiriwa kati ya watu 500,000 na milioni tatu waliuawa. Kulingana na Eghosa Osaghae, profesa wa siasa linganishi katika chuo kikuu cha Ibadan, sababu zilizopelekea vita hivi hazijabadilika mpaka hii leo.

"Watu wanadhani upande wa kusini-mashariki ndiyo ulioko katika hali ngumu na dhaifu zaidi kimamlka. Na hilo linaweza kuwa linatokana na athari za vita hivyo. Lakini hizo zote ni dhana tu," anasema Profesa Osaghae.

Na wakati huo huo, mamilioni ya watu nchini humo bado wanahamahama. Mabadilishano kati ya jamii mbalimbali za kikabila yamekuwepo wakati wote na yalirejeshwa mara baada ya vita hiyo. Msumkumo wa hili ni biashara. Wahaussa wengi wanaishi kwenye barabara ya Ogui katika mji wa Enugu. Kiongozi wao anaitwa Abubakar Yusuf Sambo, ambaye familia yake ilikwenda Enugu kutokea jimbo la kaskazini-mashariki la Adamawa miaka 100 iliyopita.

"Baada ya vita, watu wengi walirejea haraka kutoka kaskazini, kama watu wa kabila la Igbo walivyorejea kaskazini. Ni uhusiano mzuri ambao umeendelea kuwa mzuri. Lakini hadi hivi karibuni, watu wameendelea kudai uhuru," anasema Sambo na kuongeza kuwa hilo linapaswa kufanywa kwa njia za kisheria na ustarabu.

Hata kwa ngazi binafasi, Sambo anasema hajawahi kushuhudia chuki ya kikabila dhidi yake kwa sababu yeye ni Mhaussa. "Nilikulia hapa, nikasomea hapa na nina marafiki zaidi mjini Enugu kuliko niliyo nao Adamawa," anasema.

Mapambano ya kuwania rasilimali

Siasa za ndani ya Nigeria pia ni za mihemko. Moja ya sababu za vita hivyo lilikuwa suala la urari wa madaraka nchini humo. Hivi sasa mapambano ya kuwania madaraka yameshika kasi, anasema profesa Eghosa Osaghae, na kuongeza kuwa vita hivyo vya wenyewe kwa wenyewe vimeendelea kuunda uhusiano ndani ya Nigeria, na hili linashuhudiwa katika ugawaji wa nafasi za kisiasa na nafasi za juu katika taasisi za serikali.

Nigeria Abubakar Yussuf Sambo
Abubakar Yussuf Sambo anatumai Biafra haitaisambaratisha Nigeria.Picha: DW/K. Gänsler

Mwaka uliyopita, raisi Muhammadu Buhari alituhumiwa kwa kuwapendelea watu wanaotokea kaskazini. Vyama vikuu vya APC na PDP, pia vinachukuwa tahadhari wakati wa kuchaguwa wagombea wa urais kuhakikisha kwamba wagombea hao wanawakilisha Kaskazini na Kusini - na kwa maana hiyo Uislamu na Ukristu.

Lakini yote hayo hayajaleta umoja, na kinyume chake, watu kutoka jimbo la zamani la Biafra wanakosoa ukweli kwamba hadi hii leo hakujawa na rais kutoka kabila la Igbo. Wengi wanahisi kutwezwa, jambo linalocheza vizuri mikononi mwa wanaotetea uhuru, hasa mavuguvugu kama "Watu huru wa Biafra" IPOM ambalo limepata wafuasi, ingawa shughuli zake zimepungua pakubwa tangu mahakama ilipoitangaza IPOM kuwa kundi la kigaidi mnamo mwaka 2017.

Hisia vs uhalisia

Takwimu zinaonesha hali tofauti: Katika faharasi ya maendeleo ya kitaifa ya mwaka 2015, ambayo ndiyo ya karibuni zaidi, zoni za kijiografia za kusini-mashariki na kusini-kusini - ambazo ni uainishaji wa serikali wa eneo sawa na la Biafra wakati huo), ziko mbali kielimu, usawa wa kijinsia na upunguzaji wa umaskini na ziko katika nafasi nzuri zaidi kuliko zile za kaskazini.

Hisia na uhalisia huwa vinatofautiana, anasema profesa Osaghae. "Watu wengi kutoka kusini-mashariki hawaijui kaskazini hata kidogo. Wanadhani upande wa kaskazini unapata sehemu kubwa ya rasilimali za taifa. "Suala kuu, kama ilivyokuwa kabla ya vita, ni mafuta kutoka Kusini-mashariki.

Kwa upande wa sera ya kigeni ya Nigeria, vita hivyo viliacha mkururo mdogo. Biafra ilitambuliwa na mataifa machache tu, yakiwemo Tanzania, Gabon, Ghana na Cote di'voire. Pia iliungwa mkono na Vatican. Mashirika kadhaa ya kikristu, yakiwemo Caritas na Diakonishes Werk ya Ujerumani, pia yalitoa msaada kwa watu waliokwama katika vita hivyo.

Nigeria Kriegsmuseum Umuahia
Ndege iliyotumiwa katika vita ya Biashara ikiwa kwenye makumbusho ya vita ya Umuhia.Picha: DW/K. Gänsler

Serikali ya Marekani ilijaribu kupatanisha kati ya Nigeria na papa Januari 1970, lakini uhasama ulidumu kwa muda mfupi tu, anasema Nicholas Omenka, padri wa Kikatoliki na profesa wa historia katika chuo kikuu cha jimbo la Abia. Baada ya hapo, anasema, ilikuwa na Vatican na Kanisa vilivyosaidia zaidi kuijenga upya Nigeria.

Washirika wapya

Licha ya hayo, Biafra imepelekea ushirika mpya. Wakati wa vita baridi, Uingereza na Umoja wa Kisovieti kwa pamoja ziliunga mkono upande wa Nigeria. Vita vya wenyewe kwa wenyewe viliiwezesha Nigeria kuiomba Urusi na kundi la mataifa ya Ulaya Mashariki kuipatia silaha, anasema Eghisa Osaghae, uhusiano uliodumu hadi hii leo.

Chanzo: DW