1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ndege za kivita zashambulia maeneo ya waasi Yemen

Bruce Amani
16 Mei 2019

Ndege za kivita za muungano wa kijeshi unaoongozwa na Saudi Arabia zimefanya leo mashambulizi katika maeneo yanayodhibitiwa na waasi nchini Yemen ukiwemo mji mkuu Sanaa.

https://p.dw.com/p/3Ic5R
Jemen Sanaa Luftangriffe der Saudis
Picha: Reuters/M. al-Sayaghi

Hii ni baada ya waasi hao kufanya mashambulizi ya ndege zizisoruka na rubani na kuharibu bomba muhimu la mafuta, ambayo serikali ya Saudia imesema yalitokana na amri ya hasimu wake mkuu Iran. Bruce Amani na ripoti kamili))

Mashambzulizi hayo mapya yamekuja baada ya mjumbe wa Umoja wa Mataifa Martin Griffiths, ambaye amekuwa akiongoza juhudi za kumaliza mzozo huo uliodumu kwa zaidi ya miaka minne katika nchi hiyo maskini kabisa ya ulimwengu wa Kiarabu, kuonya kuwa bado inakabiliwa na kitisho cha kutumbukia katika vita kamili.

Muungano wa kijeshi unaoongozwa na Saudia, na ambao umekuwa ukipambana na wahouthi tangu Machi 2015, umethibitisha kuwa ndege zake za kivita zinafanya mashambulizi katika maeneo yote yanayokaliwa na waasi.

Duru za hospitali moja ya mji mkuu Sanaa zimesema kuwa shambulizi lililofanywa katika kitongoji kimoja cha Sanaa liliwauwa watu sita na kuwajeruhi 10. Huyu hapa mmoja wa maafisa wa ouokozi akizungumzia mashambulizi hayo "kuna msichana ndani, hatujui ni chumba kipi alichofukiwa kwenye vifusi. Kuna karibu wahanga saba au nane walioko ndani ya nyumba hiyo, kwa sasa wamepooza hawawezi kuzungumza wala kutembea. wote ni wa kutoka familia moja"

Konflikt im Jemen Versammlung von Huthi-Rebellen in Sanaa
Wapiganaji wa Kihouthi wanaungwa mkono na IranPicha: picture-alliance/dpa/H. Al-Ansi

Muungano huo ulifanya jumla ya mashambulizi 11 katika mji mkuu miongoni mwa 19 yaliyofanywa kote katika maeneo ya waasi.

Naibu waziri wa ulinzi wa Saudia Khalid bin Salman amedai kuwa shambulizi dhidi ya bomba la mafuta lilifanywa kutokana na amri ya Iran.

Waasi walisema kuwa mashambulizi yao yalikuwa ni jibu kwa uhalifu unaofanywa na Saudia katika vita vya umwagaji damu nchini Yemen, ambao umekosolewa kila mara na Umoja wa Mataifa na makundi ya haki za binaadamu.

Naibu waziri wa mambo ya nchi za kigeni wa Saudi Arabia Adel al-Jubeir amesema kuwa waasi wa Houthi wanayatoa kafara mahitaji ya watu wa Yemen kwa manufaa ya Iran. 

Naye Anwar Gargash waziri wa mambo ya nchi za kigeni wa Umoja wa Falme za Kiarabu, ambayo ni mshirika mkuu alionya kuwa watalipiza kisasi vikali sana wakati wakiona Wahouthi wakiyalenga makaazi ya raia kama kilichotokea Saudi Arabia.

Waangalizi wa Umoja wa Mataifa wamethibisha Jumanne wiki hii kuwa wapiganaji wa Kihouthi wameondoka katika bandari ya Hodeidah na nyingine mbili za Bahari ya Shamu