Mtawala wa muda wa kijeshi wa Misri Hussein Tantawi afariki
21 Septemba 2021Tantawi aliyeliongoza baraza la kijeshi lililoitawala Misri kwa kipindi cha mwaka mmoja na nusu baada ya vuguvugu la harakati za wananchi lililomuondoa madarakani rais wa muda mrefu Hosni Mubarak mwaka 2011, amefariki akiwa na umri wa miaka 85.
Tantawi aliyeangaliwa kama mkongwe wa vita vyote vya Misri dhidi ya Israel katika miaka ya 1956, 1967 na 1973 alishikilia nafasi ya waziri wa ulinzi kwa takriban miaka 21.
Rais Abdel Fattah al Sisi amesikitishwa na kifo cha Tantawi ambapo katika taarifa yake ametowa salamu za pole kwa familia yake.
Rais Sisi kupitia taarifa hiyo amesema Tantawi alikuwa kiongozi na mzee wa taifa aliyechukuwa jukumu la kuiongoza Misri wakati wa kipindi kigumu ambapo alitumia hekima na uwezo kuzikabili hatari zilizokuwa zimeizunguuka nchi hiyo.