1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mkurugenzi wa zamani wa Oxfam Haiti akiri kuwaajiri makahaba

19 Februari 2018

Afisa wa zamani wa Shirika la Oxfam anayehusika kwenye kadhia ya ukahaba amekiri kulipia ngono katika makaazi yake wakati wa uchunguzi wa ndani juu ya madai ya unyanyasaji wa kingono yaliyotolewa hivi karibuni

https://p.dw.com/p/2suyt
Uk Oxfam-Sex-Skandal | Logo
Picha: Getty Images/AFP/A. Buchanan

Ripoti  iliyotolewa hii leo imeelezea kuwa wafanyakazi watatu wa shirika la misaada la Uingereza Oxfam pia walimtisha na kumpiga shahidi katika uchunguzi wa madai ya visa vya unyanyasaji wa kingono nchini Haiti kufuatia tetemeko baya la ardhi lililotokea huko mwa 2010. Shirika hilo liliwafuta kazi wafanyakazi wanne na kuruhusu wafanyakazi wengine watatu akiwemo aliyekuwa mkurugenzi wa shirika hilo nchini Haiti Roland van Hauwermeiren, kujiuzulu kufuatia madai ya kwamba aliwaajiri watu wanaojiuza kingono walio na umri mdogo.

Hata hivyo Hauwermeiren  aliye na miaka 68 mwenye asili ya Ubelgiji, amekana kuandaa sherehe za kingono au kuingia kwenye madanguro katika kisiwa hicho cha Caribbean, akisema kwamba aliliambia shirika la Oxfam ameshawahi kujihusisha na mahusiano ya kimapenzi mara tatu nyumbani kwake lakini hakuwahi kulipia huduma hiyo huku akisema kwamba anajutia na kuona aibu kushiriki tukio hilo. 

Haiti Hilfe durch Oxfam
Picha: picture-alliance/dpa/Oxfam/F. Afonso

Aidha nakala ndefu iliyotolewa mwaka wa 2011 na kuwekwa hadharani na shirika la Oxfam ilisema Van Hauwermeiren aliomba kujiuzulu baada ya kukiri kwa wachunguzi kuwa aliwaajiri watu wanaojiuza kingono katika makaazi yaliyokuwa yanalipiwa na shirika hilo.

Oxfam kwa sasa limeweka wazi mpango wake wa kupambana na masuala ya unyanyasaji wa kingono na kukubaliana kutoitisha fedha zozote za serikali hadi pale mabadiliko yatakapofanyika. Shirika hilo limeshutumiwa kwa kutokuwa wazi juu ya matukio hayo ya unyanyasaji wa kingono hatua iliyosababisha kujiuzulu kwa naibu wa shirika hilo na baadhi ya mabalozi wake kama Desmond Tutu.

Wakati huo huo shirika hilo la Oxfam limesema limetoa ripoti yake ili kuwa wazi iwezekanavyo juu ya hatua iliyofikiwa wakati wa uchunguzi na kuonyesha uaminifu uliovunjwa kati ya shirika hilo na wafanyakazi wake. 

Tayari majina ya wwanaume saba wanaodaiwa kutekeleza visa hivyo vya unyanyasaji wa kingono yamepelekwambele ya mamlaka husika na ripoti kamili kupelekwa kwa  kwa balozi wa Haiti mjini London. Shirika hilolimeongeza kuwa nakala  ya ripoti hiyo pia itapelekewa  serikali ya Haiti iliyosema itaanzisha uchunguzi juu ya suala hilo katika mkutano uliopangiwa kufanyika hii leo.

Mwandishi: Amina Abubakar/AFP/AP

Mhariri: Yusuf Saumu