1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mapigano mapya yaripotiwa katika jimbo la Afar, Ethiopia

Amina Mjahid
13 Oktoba 2021

Duru kutoka mashirika ya kutoa misaada ya kiutu na waasi Ethiopia, zimesema mapigano yameanza tena katika jimbo la Afar Kaskazini mwa nchi hiyo, baada ya mwezi mzima wa utulivu.

https://p.dw.com/p/41cBE
Äthiopien Mekele | Pro-TPLF Rebellen
Picha: YASUYOSHI CHIBA/AFP

Kulingana na duru za mashirika ya misaada ya kiutu, kumeripotiwa mapigano katika mji wa Awra kwenye jimbo la Afar, yaliyojumuisha matumizi ya silaha nzito kutoka kwa kundi la wapiganaji la Tigray TPLF yaliyosababisha mauaji ya wakaazi wengi. 

Hata hivyo ripoti hiyo haikuweza kudhibitishwa maana maafisa wa serikali katika jimbo la Afar hawakupatikana kutoa maoni yao. Msemaji wa TPLF Getachew Reda amekanusha madai kuwa waasi walitumia silaha nzito dhidi ya wakaazi lakini akathibitisha kuwepo mapigano makali Afar.

soma zaidi: Abiy Ahmed aapishwa kwa muhula mpya kuongoza Ethiopia

Kwa takriban wiki moja duru hizo zimekuwa zikiripoti dalili zinazoonesha mashambulizi yanayofanywa na serikali yanayoweza kuanzisha tena vita vilivyodumu miezi 11 Kaskazini mwa Ethiopia.  

Serkali yaahidi kuwalinda raia dhidi ya matendo ya ugaidi

Äthiopien | Premierminister Abiy Ahmed Ali
Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed Picha: Office of the Prime Minister Ethiopia/UPI Photo/Newscom/picture alliance

Maafisa wa serikali hawazungumza wazi iwapo kweli wanalishambulia eneo hilo lakini ofisi ya Waziri Mkuu Abiy Ahmed ilisema wiki hii kwamba, ina jukumu la kuwalinda raia wake katika maeneo yote ya nchi dhidi ya matendo yoyote yakigaidi. 

Mapigano yalianza mwezi Novemba mwaka jana wakati Abiy alipotuma wanajeshi wake kuuangusha utawala wa TPLF katika jimbo la Tigray. Kundi hilo liliwahi kudhibiti siasa za taifa, kabla ya Abiy kuchukua madaraka mwaka 2018. Abiy ambaye ni mshindi wa tuzo ya amani ya Nobel mwaka 2019 amesema hatua yake ilitokana na mashambulizi ya TPLF dhidi ya makambi ya kijeshi. 

Vikosi vya serikali viliwaondoa wapiganaji wa TPLF kutoka katika miji ya jimbo la Tigray lakini baadae TPLF wakaiteka tena miji hiyo ikiwemo mji mkuu wa Tigray Mekele mwishoni mwa mwezi Juni.  

soma zaidi: TPLF yasema jeshi la Ethiopia limeanza operesheni Tigray

Mwezi Julai kundi hilo likosagea katika majimbo ya Afar na Amhara hatua waliyosema ni ya kuvizuwiya vikosi vya serikali kujikusanya wakitaka kupinga kile walichosema ni mzingiro unaolenga kuzuwiya misaada ya kiutu kufika katika eneo hilo ambako Umoja wa Mataifa unakadiria maelfu wanakabiliwa na hatari ya njaa.

Maafisa wa UN warejeshwa kutoka Ethiopia kwa kuwakosoa wakuu wao

Huku hayo yakiarifiwa maafisa wawili wa juu wa Umoja wa Mataifa wamerejeshwa kutoka Ethiopia baada ya rekodi ya sauti kusikika inayowakosoa maafisa wakuu wa Umoja huo iliyotolewa mitandaoni, hii ikiwa ni kwa mujibu wa barua na msemaji wa shirika la idadi ya watu la Umoja wa Mataifa UNFPA. 

Antonio Vitorino KOMMENTARBILD
Mkuu wa shirika la uhamiaji la Umoja wa Mataifa IOM, Antonio Vitorino

Katika sauti hizoo zilizorekodiwa, wanawake wawili ambao hawakutajwa jina, waliosema wanafanya kazi na Umoja wa Mataifa Ethiopia,  walimuambia muandishi habari kuwa baadhi yamaafisa wa juu ya Umoja wa Mataifa, wanavihurumia vikosi vya TPLF Kaskazini mwa nchi hiyo wanapambana na vikosi vya serikali. 

Katika barua ya terehe 11 Oktoba, mkuu wa shirika la uhamiaji la Umoja wa Mataifa IOM, Antonio Vitorino alisema mfanyakazi mmoja alirejeshwa makao makuu na kuwekwa likizo ya muda wakisubiri uchunguzi wa rekodi hizo. 

Chanzo: afp/reuters