Mambo yameiendea kombo Dortmund
15 Agosti 2011Sejad Salihovic kwa niaba ya Hoffenheim aliikaribisha Dortmund kwa bao hilo kunako dakika 9 ya mechi hiyo na timu hiyo bingwa hadi kumalizika mechi hiyo ilishindwa kuonyesha umahiri wake kama ilivyokuwa katika mechi yake ya ufunguzi ilipoifunga Hamburg mabao 3-1.
Hata kwa mchezaji nyota wa timu hiyo Dortmund, Mario Goetze, aliyechangia ushindi huo dhidi ya Hamburg pamoja na katika mechi ya kirafiki kati ya Ujerumani na Brazil, alishindwa kufanya miujiza yake kama kawaida na Dortmund iliishia kufungwa na Hoffenheim kama ilivyokuwa msimu uliokwisha.
Ama kwengineko mambo yalionekana kuwa sio mabaya kwa timu kuu Ujerumani, Bayern Munich, baada ya kupata bao moja la bahati dhidi ya Wolfsburg. Mtobwe wa Luiz Gustavo aliousukuma wavuni mwa Wolfsburg ndiyo ulioipa ushindi wa pointi 3 timu hiyo, ambazo winga Franck Ribery, anasema ni muhimu mno kwao.
Ushindi wa dakika za mwisho pia uliiangukia timu ya Bayer Leverkusen dhidi ya Werder Bremen hapo jana kutoka kwake Michal Kadlec. Timu hizo mbili ni miongoni mwa timu nane zilizo na pointi 3.
Kocha wa Leverkusen Robin Dutt siku ya Ijumaa alisema kuwa hakuna nafasi ya Ballack na Rolfes kucheza kwa wakati mmoja kwenye timu hiyo na ndiyo sababu aliamua kumpa Ballack nafasi kwanza katika mechi hiyo na baadaye alifanya mabadiliko na kumuingiza Rolfes aichukuwe nafasi ya Ballack, na Rolfes hakuchelewa kutoa pasi safi kwa Kadlec aliyelifunga bao hilo la ushindi.
Katika mechi nyengine hapo jana, Kaiserslautern na Augsburg zilitoka sare ya bao 1-1.
Kaiserslautern ilijinyakulia bao la kwanza msimu huu kunako dakika 80 ya mechi hiyo na dakika sita baadaye wenyeji Augsburg walifanikiwa kulisawazisha bao hilo.
Mainz na Hannover wanaongoza ligi mpaka sasa wakiwa na pointi 6 kila mmoja.
Timu nyingine iliyozusha mshangao baada ya msimu uliopita ni Hannover ambayo iliifunga wenyeji Nuremberg kupitia mikwaju ya Mohammed Abdellaoue na Konstantin Rausch yote katika awamu ya kwanza.
Timu ya Cologne iliongoza mechi yake dhidi ya Schalke 04 kupitia mchezaji wake wa kiungo cha kati Lukas Podolski, lakini mikwaju mitatu ya Huntelaar kunako dakika 42,47, na 84, pamoja na wa Lewis Holtby kunako dakika 48, na hatimaye wa Raul Gonzales kunako dakika 59 kuliipa Schalke ushindi mkubwa mno.
Mwandishi: Maryam Abdalla/Afpe/Dpae
Mhariri:Josephat Charo