Makabiliano makali yaendelea Qusayr, Syria
20 Mei 2013Duru za kuaminika zinasema wapiganaji wa Hezbollah wanaoshirikiana na wanajeshi wa utawala wa Rais Bashar al Assad wamekuwa wakikabiliana na waasi kwa wiki moja sasa katika eneo la Qusayr ambalo ni muhimu kwa sababu inaunganisha Damscus na pwani ya nchi hiyo na pia iko mpakani na Lebanon.
'Shirika la kutetea haki za binadamu nchini humo lenye makao yake nchini Uingereza limesema karibu watu 55 wameuwawa katika mji huo wengi wao wakiwa ni waasi mbali na wapiganaji wa Hezbollah na wanejeshi wa serikali. Kulingana na shirika hilo ambalo linategemea taarifa na takwimu kutoka kwa wanaharakati,madaktari na wanasheria walioko nchini humo kiasi ya watu 94,000 wameuwawa tangu mzozo wa Syria kuanza mwezi Machi mwaka 2011.
Uvamizi huo wa jeshi katika mji wa Qusayr ulianza jana huku wapinzani wa Assad wakionya kuwa mashambulio ya kinyama katika mji huo huenda ukadidimiza juhudi za Marekani na Urusi za kuandaa mkutano wa amani unaonuia kumaliza vita hivyo vilivyosababisha vifo vya maelfu ya wasyria.
Jumuiya ya nchi za kiarabu imeitisha mkutano wa dharura siku ya Alhamisi wiki hii kabla ya mkutano huo wa amani huku baraza la kitaifa la upinzani Syria likitaka jumuiya hiyo kukutana na kumaliza kile ilichokiita mauaji ya halaiki mjini Qusayr.
Huku hayo yakijiri,eneo la Golan linalokaliwa na Israel limelengwa kwa risasi kutoka Syria usiku wa kuamkia leo lakini hakuna majeraha au uharibifu ulioripotiwa. Kulingana na msemaji wa kijeshi wa Israel ufyatuaji huo ulikuwa wa kutumia silaha ndogo na unaaminika haukulenga milima hiyo kimakusudi.
Rais Assad atilia shaka mkutano wa amani
Hata hivyo msemaji huyo hakuthibitisha ripoti za vyombo vya habari vya eneo hilo kuwa silaha hizo zilifyatuliwa karibu na kituo cha kushika doria cha kijeshi.Jeshi la Israel halikujibu mashambuli hayo na tayari Israel imewasilisha lalamiko kwa kikosi cha Umoja wa mataifa kilichoko katika eneo hilo.
Na shirika la kimataifa la misaada la Oxfarm limetoa wito wa misaada zaidi kusaidia wakimbizi wa Syria walioko Lebanon na Jordan na kuonya kuwa hali ya hewa ya sasa itaongeza madhara ya kiafya kutokana na ukosefu wa makaazi, maji na maeneo ya kujisaidia huku mapigano kati ya wanajeshi wa serikali wanaosaidiwa na wanamgambo wa Hezbollah dhidi ya ngome za waasi yakichacha nchini Syria.
Shirika la Oxfarm limesema linahitaji dola milioni 53 ili kuboresha huduma za maji na usafi kwa ajili ya wakimbizi wa Syria na kufikia sasa shirika hilo limepata msaada wa dola milioni 10.6. Shirika hilo limesema kuwa kuharisha na magonjwa ya ngozi yameanza kuonekana miongoni mwa wakimbizi hao walioko Jordan na Lebanon. Nchi hizo mbili zinawahifadhi wakimbizi milioni 1.5 ambao wamekimbia vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini mwao. Oxfarm imesema inahitaji ufadhili huo haraka iwezekanvyo kwa sababu viwango vya joto vinatarajiwa kupanda katika wiki chache zijazo katika eneo hilo.
Mwandishi:Caro Robi/ap/afp
Mhariri: Daniel Gakuba