Magenge ya wahalifu yakabiliana na polisi Haiti
10 Oktoba 2025
Wanachama wa magenge ya wahalifu wamekabiliana na polisi siku ya Alhamisi karibu na makao makuu ya serikali ya Haiti wakati mawaziri wanaoendesha utawala dhaifu wa muda walipokuwa wakikutana kwa mara ya kwanza baada ya miezi kadhaa.
Shirika la habari la AFP na shahidi walithibitisha milio ya risasi katika mji mkuu Port-au-Prince karibu na Ikulu ya Kitaifa. Jengo hilo lilikuwa limetelekezwa kwa sababu eneo hilo lilionekana kuwa hatari sana lakini baraza la mawaziri lilikutana hapo jana ili kujaribu kuleta hali ya kawaida na utulivu.
Haiti inayokumbwa na umaskini haina bunge wala rais na haijafanya uchaguzi tangu 2016. Magenge yaliyojihami vyema yanadhibiti sehemu kubwa ya nchi licha ya kutumwa kwa kikosi cha kimataifa kinachoongozwa na Kenya.
Ofisi ya Waziri Mkuu Alix Didier Fils-Aime ilitoa taarifa ikisema mkutano huo uliashiria "awamu ya ishara na madhubuti" katika serikali kuchukua tena udhibiti wa kati Port-Au-Prince.
Mwandishi wa AFP na shahidi mwingine walisikia milio ya risasi karibu na Ikulu ya Kitaifa wakati mkutano ukiendelea. Polisi na magari ya kivita yalishika doria mitaani.
Serikali haikusema mara moja ikiwa mtu yeyote alijeruhiwa au kuuawa.