1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Licha ya kuuawa Sotloff, Obama harudi nyuma

Mohammed Khelef3 Septemba 2014

Rais Barack Obama wa Marekani amesema serikali yake haitarudi nyuma kwenye operesheni yake dhidi ya magaidi wanaojiita Dola la Kiislamu, licha ya wanamgambo hao kumuua mateka mwengine wa Kimarekani.

https://p.dw.com/p/1D5j7
Mwandishi wa habari wa Marekani, Steven Sotloff, aliyekatwa kichwa na waasi wa Dola la Kiislamu.
Mwandishi wa habari wa Marekani, Steven Sotloff, aliyekatwa kichwa na waasi wa Dola la Kiislamu.Picha: picture-alliance/dpa

Akizungumza mjini Tallin, Estonia, akiwa mwanzoni mwa ziara yake Ulaya ya Mashariki, Rais Obama amesema licha ya vitisho vinavyotolewa na magaidi wa Dola la Kiislamu kwa kuwauwa raia wa nchi yake, serikali yake haitarudi nyuma.

"Chochote ambacho wauaji hawa wanatazamia kukifanikisha kwa kuwauwa Wamarekani wasio hatia kama Steven Sotloff, basi wameshahindwa, kwani kama walivyo watu wengine duniani, Marekani inakerwa na unyama wao, hatutoshika na vitendo vyao vya kikatili vinatuunganisha kama nchi na kutuchochea kupambana na magaidi hawa."

Obama alitumia mkutano wake na waandishi wa habari kutoa pole kwa familia ya Sotloff. Tayari Marekani imethibitisha kuwa vidio iliyosambazwa jana mtandaoni ikimuonesha Sotloff akinyongwa ni ya kweli.

Kwa mujibu wa msemaji wa Baraza la Usalama la Marekani, Caitlin Hayden, mashirika ya ujasusi ya nchi hiyo yameihakiki vidio hiyo na kuridhika kwamba ni ya kweli. Vidio hiyo imetumwa mtandaoni wiki mbili tu baada ya ile inayomuonesha mwandishi mwengine wa habari wa Kimarekani, James Foley, akikatwa kichwa.

Cameron aitisha kikao cha dharura

Nchini Uingereza, Waziri Mkuu David Cameron aliitisha kikao cha dharura kufuatia mauaji ya raia huyo wa Marekani. Akizungumza kabla ya mkutano huo wa dharura, Cameron aliyalaani mauaji hayo akiyaita kuwa ni kitendo cha aibu na kikatili.

Waziri Mkuu wa Uingereza, David Cameron.
Waziri Mkuu wa Uingereza, David Cameron.Picha: Reuters

"Kama ambavyo nimekuwa nikisema katika wiki za hivi karibuni, magaidi wa Dola la Kiislamu hawatambui dini. Wanawatisha Wasyria, Wairaqi, Wamarekani na Waingereza na hawajui tafauti kati ya Waislamu, Wakristo au wa imani nyengine." Alisema Cameron. Ujumbe kwenye vidio hiyo unaonya kuwa mateka wa Kiingereza, David Haines, ndiye atakayefuatia kuuawa.

Hadi sasa, Uingereza haijaungana na Marekani kwenye mashambulizi yake dhidi ya wapiganaji wa Dola la Kiislamu, lakini imesaidia kuwapa silaha Wakurdi wanaopigana kaskazini mwa Iraq na imesambaza msaada kwa watu waliokuwa wamezungukwa na kundi hilo kwenye Mlima Sinjar na mji wa Amerli.

Australia haiondoi uwezekano wa kujiunga na Marekani

Wakati haijafahamika ikiwa kikao cha Jumatano kingeliweza kuifanya Uingereza kubadili muelekeo wake kwenye kadhia hii, tayari Australia ilishasema haiondoshi uwezekano wa kutuma wanajeshi kuunga mkono mashambulizi ya anga ya Marekani dhidi ya Dola la Kiislamu. Waziri Mkuu Tony Abbott, aliwaambia waandishi wa habari kuwa mauaji ya Sotlof yanaweza kubadili hali ya mambo.

Waziri Mkuu wa Australia, Tony Abbott.
Waziri Mkuu wa Australia, Tony Abbott.Picha: picture-alliance/dpa

"Nchi nyingi zinazungumzia njia bora zaidi ya kuchukua, lakini ukweli ni kuwa Dola la Kiislamu ni kitisho sio tu kwa watu wa Mashariki ya Kati, bali kwa duni nzima. Huu ni mzozo ambao tungetaka kuuepuka, lakini kwa masikitiko unatufikia hapa tulipo, kwani kama tulivyoona kiasi cha raia 60 wa Australia wanapigana upande wa magaidi kwenye eneo hilo la dunia." Alisema Abbott.

Wachambuzi wa mambo wanaamini Marekani na washirika wake wanajitayarisha kwa vita kamili vya angani na ardhini dhidi ya wanamgambo hao, lakini ukweli kwamba watapaswa pia kuingia Syria ambako ndiko ulikoanzia uasi wa kundi hilo na ambako kwa miaka mitatu sasa wameshindwa kuafikiana kupitia Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, unaifanya hali kuzidi kuwa ngumu.

Mwandishi: Mohammed Khelef/Reuters/AP/AFP
Mhariri: Iddi Ssessanga