1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Leverkusen yapanda kileleni mwa Bundesliga

Josephat Charo
13 Desemba 2020

Winga kutoka Jamaica Leon Bailey alifunga mabao mawili wakati Bayer Leverkusen ilipoipiga kumbo Bayern Munich na kuiondoa kileleni mwa Bundeslliga kwa kuikandika Hoffenheim 4-1 Jumapili (13.12.2020)

https://p.dw.com/p/3mfCV
Fußball Bundesliga Bayer 04 Leverkusen - TSG Hoffenheim
Picha: Thilo Schmuelgen/AFP/Getty Images

Bailey alianza kufunga kupitia mkwaju maridadi mapema dhidi ya Hoffenheim wakati Leverkusen ambao walikuwa katika hali nzuri kimchezo walipopata ushindi wao wa saba msimu huu na kuwaondoa vinara wa ligi Bayern na kuushika usukani wa ligi.

Florian Grillitsch wa Hoffenheim alipiga besela kwa mpira wa kichwa baada ya sekunde 14, lakini ni Leverkusen ambao walifanikiwa kutangulia dakika ya nne. Akipasiana vyema na Nadiem Amiri, Bailey 'aliukunja' mpira pembeni juu ya lango kutoka eneo la adhabu.

Pasi ambayo haikuwa na macho kutoka kwa Andrej Kramaric ilimruhusu Bailey kufunga bao la pili muda mfupi kabla dakika 30 za mchezo kukamilika, akimzungusha kipa wa Hoffenheim, Oliver Baumann, na kuutia kimyani mpira kutoka yadi 20 lango likiwa wazi.

Baumann aliikoa timu yake aliporuka kama nyani kumnyima bao Florian Wirtz muda mfupi kabla kipindi cha mapumziko, na Christoph Baumgartner akasawazisha goli moja kupitia mkwaju aliouvurumisha kutoka mbali baada ya mapumziko.

Hata hivyo furaha ya Hoffenheim ilidumu muda mfupi pale Wirtz alipocheza chakacha kwenye kisanduku na kumvalisha kanzu Baumann dakika ya 55. Hatima ya wageni hao ilizamishwa pale Grillitsch na Stefan Posch walipotolewa nje ya uwanja baada ya kuonyeshwa kadi nyekundu katika dakika 15, na Lucas Alario akaupiga msumari wa mwisho katika jeneza la Hoffenheim kwa kupachika bao la nne kupitia mkwaju wa penalti katika muda wa ziada.

(afp)