Kim Jong Un asifu wanajeshi wa Korea Kaskazini nje ya nchi
1 Januari 2026
Kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong Un amewasifu wanajeshi wake wanaopigana katika “nchi ya kigeni” kupitia ujumbe wa Mwaka Mpya, akisisitiza ushirikiano wa Pyongyang na Moscow. Bila kuitaja moja kwa moja Ukraine, Kim aliwahutubia wanajeshi waliotumwa nje ya nchi, akiwataka wawe jasiri na kupongeza kile alichokiita utetezi wa heshima ya taifa.
Kwa mujibu wa vyombo vya habari vya serikali, Kim alisema wanajeshi hao wanaungwa mkono na Pyongyang pamoja na Moscow. Mashirika ya kijasusi ya Korea Kusini na nchi za Magharibi yanasema Korea Kaskazini imetuma maelfu ya wanajeshi kuisaidia Urusi katika vita vyake dhidi ya Ukraine, ambapo mamia wameuawa na wengine wengi kujeruhiwa.
Wachambuzi wanasema Pyongyang inapokea msaada wa kifedha, teknolojia ya kijeshi na mahitaji ya nishati kutoka Urusi. Wakati huo huo, wanajeshi wawili wa Korea Kaskazini waliokamatwa na Ukraine wameripotiwa kueleza nia ya kuanza maisha mapya Korea Kusini.